
Na James K. Mwanamyoto - Arusha
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM–TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amewataka Wakuu wa Shule za Sekondari nchini kutokuwa kikwazo cha utendaji kazi wa walimu wanaowasimamia, akisisitiza kuwa jukumu lao la msingi ni kuweka mazingira wezeshi yatakayowawezesha walimu kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi na weledi.
Prof. Shemdoe wito huo leo kwa Wakuu hao wa shule nchini, wakati akifungua Mkutano wa 20 wa Wakuu wa Shule za Sekondari Tanzania (TAHOSSA), unaofanyika Jijini Arusha katika Ukumbi wa Tanzania Convention Center (Ngurudoto Mountain Lodge).
“Walimu wakuu mmepewa hizi nafasi za uongozi ili muwaongoze na kuwasaidia walio chini yenu, hivyo msiwe vikwazo kiutendaji katika shule mnazozisimamia,” amesisitiza Prof. Shemdoe.
Prof. Shemdoe amesema, haipendezi kwa Mkuu wa shule unapoonekana mwalimu wa taaluma anatafuta njia tofauti ya kupita ili kukukwepa, wakati mwalimu mkuu anapaswa kuwa na mahusiano mazuri na walimu, mahusiano ambayo yatajenga umoja na ari ya walimu katika kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi na weledi.
Prof. Shemdoe amewataka Wakuu wa Shule nchini, kuhakikisha wana vilinda vyeo vyao kwa kufanya kazi vizuri na kwa ushirikiano na watumishi walio chini yao, wakiwemo wanafunzi pamoja na wazazi ili wasiwe sababu ya walimu, wanafunzi na wazazi kukosa tabasamu.
Aidha, Prof. Shemdoe amewaasa Wakuu hao wa shule nchini kutogeuza huduma ya elimu kuwa chanzo cha kujiingizia kipato kwa njia ya rushwa, akitoa mfano wa suala la uhamisho wa walimu na wanafunzi kutokuwa chanzo walimu wao kuomba au kushawishiwa kupokea rushwa.
Akizungumza kabla ya kumkaribisha Mgeni rasmi Prof. Shemdoe kufungua mkutano huo, Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu-TAMISEMI anayeshughulikia elimu Bw. Atupele Mwambene amesema kuwa, wakuu wa shule waliohudhuria mkutano huo wako 3500 ambao wanajukumu la msingi la kusimamia malezi ya walimu zaidi ya 100,000 ambao ndio wenye jukumu la kupeleka tabasabu kwa wanafunzi zaidi ya bilioni 5 kote nchini, kupitia utekelezaji wa majukumu yao hususani jukumu la usimamizi wa malezi na ujifunzaji kwa wanafunzi hao.
Kwa upande wake, Rais wa Wakuu wa Shule za Sekondari Tanzania (TAHOSSA) Bw. Denis Otieno amesema kwamba, wanatambua na kuthamini mchango na azma ya Serikali kuleta maendeleo katika Sekta ya Elimu, miundombinu na afya, hivyo Wakuu wa shule wataendelea kuunga mkono jitahada za Serikali kwa kutekeleza majukumu yao ipasavyo ili kuleta mapinduzi katika sekta ya elimu.
Kaulimbiu ya Mkutano Mkuu huo wa 20 wa Wakuu wa Shule za Sekondari Tanzania Bara wa mwaka 2025 unaofanyika jijini Arusha kwa siku tatu inavyosema: “Teknologia na mafunzo wa ufundi stadi katika kuimarisha ujasiliamali mjini”.






No comments:
Post a Comment