
Na Mwandishi Wetu - Dodoma
KAMISHENI ya Tume ya Madini imeridhishwa na kasi ya ukusanyaji wa maduhuli katika Sekta ya Madini kupitia Tume ya Madini, hatua inayotoa matarajio ya Serikali kuvuka lengo la kukusanya shilingi trilioni 1.2 kwa mwaka wa fedha 2025/2026.
Hayo yamebainishwa leo Mei 4, 2026 jijini Dodoma wakati Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Dkt. Janet R. Lekashingo, alipoongoza kikao cha Kamisheni kilicholenga kupokea na kujadili taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya Tume kwa kipindi cha miezi mitatu pamoja na kuweka mikakati ya kuendelea kuimarisha mchango wa Sekta ya Madini katika uchumi wa Taifa.
Akizungumza katika kikao hicho, Dkt. Lekashingo amewapongeza watendaji wa Tume ya Madini kwa mafanikio yaliyopatikana hususan katika ukusanyaji wa maduhuli, usimamizi wa masoko ya madini na vituo vya ununuzi wa madini, kuimarika kwa usalama migodini pamoja na kuongezeka kwa ushiriki wa Watanzania katika Sekta ya Madini.
“Nina imani kwa kasi iliyopo tutavuka lengo la Serikali la ukusanyaji wa maduhuli kwa mwaka huu wa fedha. Kazi inayofanywa na watendaji wa Tume inaonesha dhamira ya dhati ya kukuza Sekta ya Madini,” amesema Dkt. Lekashingo.
Kwa mujibu wa Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Mhandisi Ramadhani Lwamo, katika kipindi cha miezi mitatu iliyopita Tume imeendelea kusimamia utoaji na ufuatiliaji wa leseni za madini, ukusanyaji wa maduhuli ya Serikali, usimamizi wa uzalishaji na mauzo ya madini pamoja na utekelezaji wa majukumu ya kisheria katika sekta hiyo.
Amesema Tume pia imefanya kaguzi katika migodi mikubwa, ya kati na midogo, mitambo ya uchakataji na uchenjuaji wa madini, mabwawa ya kuhifadhi tope sumu, maeneo ya miambataka na maghala ya kuhifadhi baruti katika mikoa yote ya kimadini nchini kwa lengo la kuhakikisha shughuli za uchimbaji zinafanyika kwa kuzingatia usalama, afya na utunzaji wa mazingira.
Aidha, ameeleza kuwa usimamizi wa biashara ya madini umeendelea kuimarika kupitia masoko ya madini 44 na vituo 120 vya ununuzi wa madini vilivyoanzishwa nchini, hatua iliyosaidia kuongeza uwazi wa biashara na mapato ya Serikali.
Katika hatua mpya ya kimkakati, Kamisheni imesisitiza umuhimu wa kuwekeza katika mafunzo ya kisasa na ya kitarajio (futuristic training) kwa watumishi wa Tume ya Madini ili kuwawezesha kukabiliana na mabadiliko ya haraka ya teknolojia na mahitaji ya kimataifa, hususan katika usimamizi wa madini mkakati (critical minerals) kama vile lithium, nickel na cobalt.
Imeelezwa kuwa, ili Tanzania inufaike kikamilifu na rasilimali hizi muhimu katika uchumi wa dunia unaoelekea kwenye nishati safi na teknolojia za kisasa, ni lazima watumishi wa Tume wawezeshwe kitaaluma katika maeneo ya uchambuzi wa data za kijiolojia, matumizi ya teknolojia za kidijitali, ufuatiliaji wa minyororo ya thamani ya madini, pamoja na mifumo ya kisasa ya udhibiti wa biashara na utoroshaji.
Kamisheni imebainisha kuwa mafunzo hayo yanapaswa kuwa endelevu, shirikishi na yanayolenga kujenga uwezo wa watumishi kuwa wasimamizi wabunifu (proactive regulators) badala ya wasimamizi wa kawaida (reactive regulators), ili kuhakikisha Tanzania ina nafasi imara katika ushindani wa kimataifa wa madini mkakati.
Katika kikao hicho, Kamisheni pia imejadili changamoto mbalimbali zinazoikabili Sekta ya Madini na kuweka mikakati kupitia Kamati za Ufundi, Rasilimali Watu, Fedha na Ushirikishwaji wa Watanzania ili kuboresha mazingira ya wachimbaji na kuongeza mchango wa sekta hiyo katika Pato la Taifa.
Katika hatua nyingine, Dkt. Lekashingo amewataka watendaji kuendelea kuimarisha tafiti za madini ya kimkakati na mifumo ya kudhibiti utoroshaji wa madini ili kuhakikisha rasilimali za madini zinaendelea kuwanufaisha Watanzania na kuchochea maendeleo ya uchumi wa nchi.









No comments:
Post a Comment