WAZIRI AWESO ATOA MUELEKEO UENDELEZAJI RASILIMALI ZA MAJI NA UBORA WA MAJI NCHINI - OKULY BLOG

Breaking

Music

Header ADS

Tuesday, May 5, 2026

WAZIRI AWESO ATOA MUELEKEO UENDELEZAJI RASILIMALI ZA MAJI NA UBORA WA MAJI NCHINI



Na Okuly Julius,OKULY BLOG,DODOMA

 

Waziri wa Maji, Jumaa Aweso, amesema Serikali inaendelea kuwekeza katika uendelezaji wa rasilimali za maji kwa kujenga miundombinu himilivu itakayokabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi, ikiwemo ukame na mafuriko.


Akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Maji kwa mwaka wa fedha 2026/2027, Aweso amesema juhudi hizo zinahusisha ujenzi wa mabwawa na miradi ya uvunaji wa maji ya mvua ili kuhakikisha upatikanaji endelevu wa huduma ya maji nchini.


Ameeleza kuwa ujenzi wa Bwawa la Kidunda unaendelea kwa lengo la kuboresha huduma ya maji katika Jiji la Dar es Salaam pamoja na Mikoa ya Pwani na Morogoro, ambapo utekelezaji wake umefikia asilimia 47.02, ukiwa na gharama ya shilingi bilioni 329.47.


Aidha, Serikali imefanikiwa kumpata mkandarasi kwa ajili ya ujenzi wa Bwawa la Farkwa, litakalosaidia kuboresha huduma ya maji katika Jiji la Dodoma na Wilaya za Chamwino, Bahi na Chemba, kwa gharama ya shilingi bilioni 312.


Katika hatua nyingine, Waziri Aweso amesema Serikali imekamilisha ujenzi wa mabwawa 11 katika maeneo mbalimbali nchini, hatua inayolenga kuimarisha upatikanaji wa maji kwa matumizi ya binadamu na shughuli za kiuchumi.


Kuhusu ubora wa maji, Aweso amesema Serikali imeendelea kuimarisha huduma hiyo kupitia ufuatiliaji wa vyanzo vya maji, uhakiki wa maji ya kunywa, udhibiti wa majitaka pamoja na kuendeleza uwezo wa maabara.


Amefafanua kuwa katika mwaka 2025/26, jumla ya vyanzo 424 vilifanyiwa uchunguzi, huku skimu 690 za maji vijijini na mitandao 351 ya maji mijini zikihakikiwa ubora wake. Pia, maabara 17 zimejengewa uwezo na saba kati yake zimeendelea kudumisha ithibati ya kimataifa.


Kwa upande wa udhibiti wa majitaka, amesema sampuli 123 kutoka mifumo 84 zilichunguzwa ili kuhakikisha maji yanayosafishwa yanakidhi viwango vinavyokubalika kabla ya kurejeshwa kwenye mazingira.


Aweso amesisitiza kuwa uhakiki wa ubora wa maji kabla ya matumizi ni muhimu katika kulinda afya za wananchi na mazingira, akitoa wito kwa wadau wote kuhakikisha wanazingatia viwango vinavyotakiwa.


“Ni wajibu wa kila mdau kuhakikisha maji yanayotumika ni salama. Vilevile, viwanda na taasisi zinazozalisha majitaka lazima yahakikishe yanatibiwa ipasavyo kabla ya kurejeshwa kwenye mazingira,” amesema Aweso.

No comments:

Post a Comment