JUMLA ya Sh bilioni 213 zimetumika kuboresha sekta ya afya, miundombinu na michezo katika Manispaa ya Temeke kupitia Mradi wa Uendelezaji wa Jiji la Dar es Salaam (DMDP).
Mradi huo wa awamu ya kwanza unaotekelezwa na DMDP chini ya usimamizi wa Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa (TAMISEMI), umewezesha ujenzi wa barabara zenye urefu wa kilomota 96 kwa kiwango cha lami na zege pamoja na ujenzi wa masoko sita ya kisasa.
Pia umewezesha ujenzi wa vituo vitatu vya mabasi, viwili vilivyopo Kijichi na Mbagala kuu vimekamilika ilihali kimoja kilichopo Buza kikitarajiwa kukamilika Februari mwaka huu.
Akizungunza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo tarehe 31 Januari 2023 katika ziara ya kutembelea miradi hiyo, Kaimu Mratibu Msaidizi wa DMDP, Adelhard Kweyamba amesema jumla ya Sh bilioni 197 sawa na asilimia 92 ya fedha za miradi hiyo, zimeshafanyiwa malipo.
Akifafanua kuhusu miradi hiyo, Kweyamba amesema katika masoko hayo sita, matano kati yake yameshakamilika huku soko moja linalojengwa katika eneo la Mbagala Zakhem likitarajiwa kukamilika mwishoni mwa Februari mwaka huu.
Amesema kuhusu ujenzi wa vituo vitatu vya mabasi, viwili kati ya hivyo ambavyo vipo Kijichi na Mbagala kuu vimekamilika huku kimoja kilichopo Buza kikitarajiwa kukamilika Februari mwaka huu.
“Katika mradi huu tuna kilomita 15 za mifereji ambayo inapita kwa wananchi kuwapunguzia adha ya mafuriko. Pia tumejenga bwawa lililopo Chang’ombe ambalo linakusanya maji na kuyatoa taratibu na kuyapeleka baharini. Bwawa hili limesaidia kupunguza mafuriko kwa wakazi wa eneo hilo pamoja na wanafunzi wa Kibasila ambao sasa hawakwami tena kuongia darasani kutokana na mvua.
“Pia tumejenga kiwanja cha mpira kilichopo Makangarawe pamoja na Mwembeyanga ambavyo vinawasaidia wananchi wa huko kufanya mazoezi. Tumejenga Kituo cha afya kimoja Buza.
“Lakini Ili kuweka jiji safi tumenunua magari 20 ya kubeba taka na makontena 65 ambayo watu wanaweka takataka zao ndipo magari yanachukua na kupeleka Pugu Kinyamwezi,” amesema.
Aidha, amesema mradi huo pia umefanikisha ujenzi wa barabara mpya ya lami ambayo inafungulia wananchi wa Temeke, Charambe kuwawezesha kwenda Uwanja wa Ndege bila kupita barabara ya Mandela na kukumbana na foleni.
Amesema barabara hiyo yenye urefu wa km 7.6, imelandana na ujenzi wa daraja na makalavati sita katika eneo la Kwa Mparange lakini pia ujenzi unahusisha stendi mpya ya Buza ambavyo vyote vimegharimu Sh bilioni 19.
Pamoja na mambo mengine amesema miradi hiyo imeongeza ufanisi na kuwezesha wa sehemu ambazo zilikuwa hazifikiki sasa zimefikika kwa urahisi.
“Mfano mifereji imesaidia kupunguza adha ya mafuriko lakini pia katika barabara zetu tumeweka taa na kupunguza uhalifu na sasa ukabaji umeisha. Wananchi nao wameongeza shughuli zao sasa wanafunga maduka saa tano au saa sita usiku,” amesema.
Amesema miradi hiyo pia imeongeza thamani ya mali kwa wananchi wa Temeke ikiwamo nyumba za makazi ambazo zimeboreshwa na nyingine kujengwa mpya za kisasa tofauti na awali.
“Hayo yote ni kwa sababu pamefikika hasa ikizingatiwa mradi umelenga kufanya maboresho kwenye makazi ya wananchi wenye kipato cha chini.
“Ingawa tulipata changamoto kidogo kwani tulipokuwa tunaipita na mitambo yetu, nyumba zilipata mtikisiko na ufa, lakini tulikuwa tunajitahidi kuzikarabati ili tuwaache kwenye hali zao nzuri,” amesema.
Aidha, amewasihi wananchi wanaonufaika na miradi hiyo kuitumia kujiendeleza kijamii na kiuchumi na kuongeza kuwa ni jukumu lao kuilinda na kutoa taarifa pale kunapotokea hujuma.
Akizungumzia baadhi ya miradi hiyo, Katibu wa Soko la Mtoni mtongani ambalo limekarabatiwa kupitia DMDP, Rajabu Hamis Jongo amesema soko hilo lililokuwa limejengwa miaka 1974 na Serikali ya awamu ya kwanza, sasa limekuwa lulu kwa wafanyabiashara wa eneo hilo.
Pamoja na kuwa na soko la kisasa, ameomba Serikali kuboresha njia ili daladala zipite katika sokoni hilo na kuwezesha wateja kushuka na kununua bidhaa.
Aidha, Meneja masoko manispaa Temeke, Anzamen Mandari, mbali na kumshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kutoa kipaumbele kwa Manispaa hiyo kunufaika na miradi hiyo, pia amesema hadi jumla wafanyabiashara 228 katika soko hilo la Mtongani wamenufaika tangu lilipofunguliwa Mei mwaka jana.
No comments:
Post a Comment