
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt.Samia Suluhu Hassan katika kipindi cha Awamu ya Sita ameleta mageuzi katika Sekta ya Utalii hasa baada ya kuitangaza nchi kupitia filamu ya Tanzania the Royal Tour na Amazing Tanzania.
Katibu Mkuu,Wizara ya Maliasili, Dkt.Hassan Abbasi ameyasema hayo leo Oktoba 20 ,2025 katika mahojiano kwenye kipindi cha Dakika 45 kinachorushwa na ITV.
"Royal Tour ilitumia bilioni 8 za Kitanzania lakini mpaka sasa tumeingiza Trilioni 9" amesisitiza Dkt. Abbasi.
Amefafanua kuwa mapato yatokanayo na utalii yameongezeka kutoka dola za kimarekani bilioni 1.3 mwaka 2021 hadi kufikia dola za kimarekani bilioni 3.9 kwa takwimu za sasa.
"Maendeleo mengine ni Tanzania ilikuwa ikipokea watalii milioni 1.5 lakini sasa inapokea watalii milioni 2.2" amesema Dkt. Abbasi.
Ameongeza kuwa katika Serikali ya Awamu ya Sita ajira zimeongezeka katika sekta ya utalii kutoka milioni 1.5 hadi 2.5 kwa ajira za moja kwa moja na milioni 3.6 zisizokuwa ma moja kwa moja ambapo idadi yake jumla ni takribani ajira milioni 5.
Aidha, amesema Serikali inaendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya kukuza sekta hiyo ikiwemo kuendelea kuibua mazao mapya ya utalii na kutangaza utalii kupitia vilabu vikubwa vya michezo duniani.
Kuhusu uhifadhi, Dkt. Abbasi ameweka bayana kuwa Serikali inaendelea kuajiri askari uhifadhi na kutumia teknolojia ya
kisasa katika uhifadhi wa wanyamapori kama matumizi ya ndegenyuki na GPS Collar kufuatilia mienendo ya wanyamapori.
Ametumia fursa hiyo kutoa wito kwa wananchi kuchangamkia fursa za uwekezaji katika sekta ya utalii ikiwemo kuwekeza katika huduma za malazi, hoteli, utamaduni n.k.





No comments:
Post a Comment