Na Okuly Julius,OKULY BLOG,DODOMA
Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji (WSDP)
imeendelea kuleta mageuzi makubwa nchini baada ya kufanikisha kukwamuliwa kwa
miradi 177 ya maji vijijini iliyokuwa imesuasua, sambamba na kuongeza wigo wa
ufadhili wa sekta ya maji kufikia zaidi ya Shilingi trilioni 1.2 kupitia vyanzo
mbalimbali vya ndani na nje ya Serikali.
Akizungumza wakati akiwasilisha makadirio ya
mapato na matumizi ya Wizara ya Maji, Waziri wa Maji Mhe. Jumaa Aweso amesema
mafanikio hayo yamepatikana kupitia usimamizi madhubuti wa WSDP ambao umeongeza
ufanisi wa utekelezaji wa miradi ya maji na usafi wa mazingira nchini.
Amesema kukwamuliwa kwa miradi hiyo 177 kumeenda
sambamba na kuimarika kwa miradi mikubwa ya kimkakati ikiwemo
Mugango–Kiabakari–Butiama, Bunda, Same–Mwanga–Korogwe pamoja na miradi ya maji
katika mikoa ya Dar es Salaam na Arusha.
Waziri Aweso amesema WSDP imeiwezesha sekta ya maji kuongeza
wigo wa upatikanaji wa fedha kutoka kwa washirika wa maendeleo, taasisi za
kifedha na mifuko ya kimataifa, hatua iliyosaidia kupunguza utegemezi wa bajeti
ya Serikali.
Ameeleza kuwa kupitia mfumo huo, sekta ya maji
imefanikiwa kuvutia na kutumia zaidi ya Shilingi trilioni 1.2 kwa ujumla
kupitia michanganyiko ya fedha za ndani na nje kwa ajili ya utekelezaji wa
miradi mbalimbali ya maji nchini.
Katika mwaka wa fedha 2025/26, sekta ya maji imenufaika na
Dola za Marekani milioni 257 kutoka Mfuko wa Mabadiliko ya Tabianchi kwa ajili
ya kutekeleza miradi 15, ikiwemo Bonde la Usangu na Mradi wa Uhimilivu wa
Mabadiliko ya Tabianchi katika Mto Mkondoa.
Aidha, Mamlaka za Maji zimepokea Shilingi
takribani bilioni 7 kutoka Serikali ya Ujerumani kupitia mpango wa IFF-OBA kwa
ajili ya kuboresha huduma za maji na usafi wa mazingira katika mikoa mbalimbali
nchini.
Waziri Aweso amesema sekta ya maji imeanza kutumia hati
fungani kama chanzo mbadala cha fedha, ambapo Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa
Mazingira Tanga ilifanikiwa kuuza Hati Fungani ya Kijani yenye thamani ya
Shilingi bilioni 53.12 na kukusanya Shilingi bilioni 54.72 sawa na asilimia 103
ya lengo.
Ameongeza kuwa Wizara inaendelea na maandalizi ya Hati Fungani ya Sekta ya Maji (Water Sector Bond) pamoja na Mkakati wa Ushirikishwaji wa Sekta Binafsi ili kuongeza uwekezaji katika sekta hiyo muhimu.
.jpeg)

No comments:
Post a Comment