Na Okuly Julius-Dodoma
SERIKALI kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa ndani na nje ya nchi, imeendelea kuwekeza katika kujenga uwezo na mazingira rafiki nchini ili kuongeza kasi ya maendeleo na matumizi ya sayansi, teknolojia na ubunifu katika kukuza uchumi, kuongeza pato la Taifa, na kuboresha maisha ya watanzania kwa ujumla.
Juhudi hizo, pamoja na mambo mengine, zinajumuisha kuandaa Sera, Kanuni, Miongozo na Mikakati madhubuti na inayoendana na kasi ya mabadiliko ulimwenguni kote na kukidhi mahitaji ya nyanja mbalimbali za kiuchumi na kijamii.
Akizungumza hii leo Agosti 25,2022 jijini Dodoma wakati akifungua Mkutano wa wadau wa kujadili na kutoa maoni juu ya Rasimu ya Sera ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu na Kiunzi cha Uratibu wa Masuala ya Ubunifu nchini,Naibu katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof.Carolyne Nombo amesema kuwa Mabadiliko makubwa ya kiuchumi na kijamii duniani kote yametokana na kutilia mkazo na kuwekeza kikamilifu katika sayansi, teknolojia na ubunifu.
"Kama ilivyo kwa nchi nyingine, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inatambua umuhimu wa sayansi, teknolojia na ubunifu kama nyenzo ya uchumi na mhimili muhimu katika kuboresha maisha ya watu wake ndio maana tupo hapa tunazijadili na kupokea maoni ya wadau lengo ni kupata mawazo ya kuboresha zaidi sekta hii ya ubunifu,"Amesema Prof.Nombo
Prof.Nombo amesema kuwa dhamira ya kuendeleza Sayansi, Teknolojia na Ubunifu imekuwa sehemu ya ajenda za nchi toka miaka ya 1960, sambamba na kuanzishwa kwa Baraza la Taifa la Utafiti wa Sayansi (UTAFITI) mnamo mwaka 1968, na kutungwa kwa Sera ya kwanza ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (ST) ya mwaka 1985,ikifuatiwa na Sera ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia ya mwaka 1996 ambayo imetumika kwa kipindi chote hadi sasa.
Aidha Prof.Nombo amesema kuwa katika kutekeleza Sera ya Sayansi na Teknolojia ya mwaka 1985, 1996 na mikakati mingine ya kuendeleza sayansi, teknolojia na ubunifu vimesaidia kuimarisha maendeleo na matumizi ya Sanyansi na Teknolojia katika sekta mbalimbali za kiuchumi na kijamii nchini na kiwango kikubwa cha mafanikio hayo kimepatikana katika kipindi cha utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia ya mwaka 1996.
"Moja kati ya mafanikio makubwa yaliyopatikana ni kuongezeka kwa Taasisi za utafiti na maendeleo nchini kutoka 18 mwaka 1961 hadi kufikia jumla ya taasisi 94 mnamo mwaka 2021,kupandishwa hadhi kwa Chuo cha Ufundi cha Dar es Salaam na kuwa Taasisi ya Teknolojia ya Dar es Salaam (1997) na Taasisi ya Sayansi na Teknolojia Mbeya (2006) kuwa Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya (2012),"Ameainisha Prof.Nombo
Na kuongeza kuwa " Kumeongezeka na Taasisi za Elimu ya Juu ambazo pia zinajihusisha na utafiti na ubunifu kutoka Chuo Kikuu kishiriki kimoja hadi kufikia Vyuo Vikuu 47 mwaka 2021,kuongezeka kwa Vituo vya bunifu na Atamizi hadi kufikia Vituo zaidi ya 45 kufikia mwaka 2022,"Ameongeza Prof.Nombo
Kwa upande wake Mhe. Jerry Silaa (Mb), ambae pia ni Mwenyekiti, Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma amesema kuwa eneo la Sayansi, Teknolojia na Ubunifu ni suluhisho tosha la tatizo la ajira lililopo nchini kwani vijana wengi watajiajiri kupitia bunifu zao.
"Ni ukweli usiopingika kuwa tatizo la ajira ni kubwa katika taifa letu tuna vijana wengi Sana wamemaliza vyuo vikuu na vya kati ila bado wapo mtaani lakini suluhu yao ni kuboresha eneo la ubunifu na kuhakikisha kuwa tunaendeleza bunifu zilizopo na kuzipeleka sokoni kwa maana ya kuzibiasharisha.
Naye Mkurugenzi, Idara ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Maulilio Kipanyula amesema mkutano huo utakuja na suluhisho katika kuibua, kutambua na kuendeleza wabunifu na bunifu zinazozalishwa katika ngazi mbalimbali nchini ikiwemo mfumo usio rasmi.
"Sisi tumeamua kufanya mapitio na mabadiliko ya Sera ya Sayansi, Teknolojia na ubunifu ya mwaka ili kuakisi mahitaji na kasi ya mabadiliko ya STU kitaifa na kidunia na ndio maana tuna siku mbili hapa za kujadiliana na kupata maoni kutoka kwa wadau nia ni kujenga eneo hili la ubunifu,"Prof.Kipanyula
Kwa upande wake Mkurugenzi wa COSTECH Dkt Amos Nungu amesema kuwa bunifu zote zinazo fanywa watahakikisha zinaendana na usalama wa watu na zinatambulika ,zinaendelezwa na kubiasharishwa.
Akizungumza katika mkutano huo muwakilishi wa UNESCO nchini Faith Shayo amesema wanaamini mapitio ya rasimu yatazingatia masuala mengine kuhusu tafiti na watafiti wa kisanyasi pamoja na kuhamasisha bunifu za ndani na kuweka utaratibu wa kuzitambua na kuzikubali ikiwemo kuboreshwa ili kuendana na mazingira halisi ya watanzania.
Kikao kazi hicho cha siku mbili kinalenga kujadili na kutoa maoni juu ya nyezo mbili muhimu ambazo ni kuandaa Kiunzi cha Uratibu wa Masuala ya Ubunifu nchini `National Innovation Framework ambapo kiunzi hiki, ni nyenzo itakayorahisisha utekelezaji wa Sera, pamoja na kuimarisha uratibu na usimamizi wa ubunifu katika ngazi mbalimbali nchini na utengamano kati ya wadau mbalimbali wa sayansi, teknolojia na ubunifu hapa nchini.







No comments:
Post a Comment