MADALALI WAPIGWA MARUFUKU KUWARUBUNI WAKULIMA-WRRB - OKULY BLOG

Breaking

Music

Header ADS

Wednesday, February 15, 2023

MADALALI WAPIGWA MARUFUKU KUWARUBUNI WAKULIMA-WRRB

Mkurugenzi Mtendaji wa BODI ya usimamizi wa Stakabadhi za ghala (WRRB) Asangye Bangu akizungumza ,wakati akielezea utekelezaji wa shughuli mbalimbali za bodi hiyo mbele ya waandishi wa habari leo Februari 15,2023,jijini Dodoma.

Na Okuly Julius-Dodoma

BODI ya usimamizi wa Stakabadhi za ghala (WRRB) imetoa wito kwa madalali kuacha tabia ya kuwarubuni wakulima na badala yake kuwaacha waingie kwenye mfumo wa Stakabadhi ghalani ili kuuza mazao yao kulingana na bei iliyopo sokoni.

Kauli hiyo imetolewa na Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi hiyo Asangye Bangu ,wakati akielezea utekelezaji wa shughuli mbalimbali za bodi hiyo mbele ya waandishi wa habari leo Februari 15,2023,jijini Dodoma.

Ambapo Bangu amesema kuwa kumekuwa na wimbi la watu wanakwenda mashambani kwa wakulima na kuwadalalia mazao na kununua kwa bei ya chini kitu ambacho kinaendelea kudidimiza maendeleo ya wakulima.

"Natoa wito kwa madalali waache kuwarubuni wakulima wawaache wajiunge katika Mfumo wa Stakabadhi ghalani ili waweze kuuza mazao yao kwa bei ya ushindani iliyopo sokoni kwa kuendelea kuuza mazao shambani inaendelea kuwadidimiza wakulima kwa sababu madalali wengi wananunua mazao kwa bei ya chini tofauti kabisa na bei iliyopo kwenye mfumo,"amesema Bangu

Bangu amesema mafanikio yaliyopatikana baada ya kuanzishwa kwa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala ni pamoja na ongezeko la bei za mazao, mapato ya mkulima na mapato ya Serikali kwa wastani wa asilimia 200% kutokana na urasimishaji, ongezeko la uzalishaji wa mazao kwa wastani wa asilimia 12% kwa mwaka,kichecheo cha ubora wa mazao yanayofikishwa sokoni,

Ametaja mafanikio mengine kuwa  ni upatikanaji wa takwimu sahihi za mazao yanayopita kwenye Mfumo wa Stakabadhi za Ghala, ongezeko la mapato ya uhakika kwa Serikali Kuu na Serikali za Mitaa na kukuza huduma za fedha vijijini,kufanikisha uanzishaji wa Soko la Bidhaa Tanzania.

Aidha, Mkurugenzi huyo amesema kuwa tangu kuanzishwa kwa Mfumo 2007/08 hadi 2020/21 ukuaji wa uzalishaji umekuwa ukiongezeka kwa wastani wa 12% kwa mwaka ikilinganishwa na ukuaji wa 2% kwa mwaka kabla ya kuanzishwa kwa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala.

"Kwa mfano katika zao la Korosho mara baada ya kuanzishwa kwa Mfumo palikuwa na ongezeko la asilimia 164% la bei kutoka Ths 350.00 msimu wa 2006/07 hadi kufikia Tsh 925.00 msimu wa 2007/08 mwaka wa kuanza wa Mfumo; katika miaka minane tokea kuanzishwa kwa Mfumo 2007/08 hadi 2014/15 wastani wa ongezeko la bei kwa mwaka ulikuwa 25% kulinganisha na ongezeko la bei miaka minane kabla ya kuanzishwa kwa Mfumo la 12% kwa mwaka kaunzia mwaka 1998/99 hadi 2006/07," amebainisha Bangu

Mkurugenzi huyo amesema kuwa ili kuendana na kasi ya ukuaji wa teknojia Bodi imekuwa ikishirikiana kwa karibu na kuhamasisha bodi ya TEHAMA kukamilisha mifumo mipya na kuhamishia huduma za Bodi hiyo kwenda kidijitali.

Aidha, Bodi imeendalea na  juhudi za kuboresha Mfumo uliokuwepo wa kizamani wa Usimamizi wa ghala, ambapo kushirikiana na Bodi ya TEHAMA inakuja na Mfumo mpya wenye kuweza kurahisisha kazi za
maandalizi ya taarifa, utoaji stakabadhi na udhibiti wa matukio ghalani hivyo kupunguza muda wa michakato na kuongeza ufanisi na usalama wa mzigo.

"Majaribio ya Mfumo wa Maombi ya Leseni Mtandaoni
yamefanyika na mapendekezo ya maboresho yamepelekwa kwa programmers kwa ajili ya kufanyiwa kazi,"amesema Bangu

Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) ni taasisi chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara iliyoundwa kwa Sheria Namba 10 ya 2005 na Marekebisho Kifungu 4 Sura 339 R.E. 2016 iliyopewa majukumu chini ya Kifungu 5 (a-j) ikiwemo kutoa leseni kwa waendesha ghala, meneja dhamana na wagakuzi wa ghala; kuchapa and kuidhinisha vitabu vya Stakabadhi za Ghala, kusajili na kuingiza taarifa za wadau muhimu wa mfumo, kuwakilisha nchi katika masuala ya taifa na kimataifa yahusuyo Mfumo wa Stakabadhi za Ghala pamoja na majukumu mengine kama taasisi itakavyoelekezwa na Mhe. Waziri wa Viwanda na Biashara.



No comments:

Post a Comment