Na Okuly Julius-Dodoma
Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Dkt Dorothy Gwajima ametoa wito kwa Wanaume na Wavulana kote nchini kubadili mitizamo na kuongeza jitihada katika mapambano ya kupinga ukeketaji dhidi ya Wanawake na watoto wa kike kwa kuwashawishi kutotamani kufanyiwa ukeketaji.
Dkt.Gwajima ametoa wito huo leo Februari 2,2023 jijini Dodoma ,wakati akizungumza na waandishi habari ,kuelekea kilele cha Maadhimisho ya siku ya kimataifa ya kupinga ukeketaji dhidi ya Wanawake na watoto wa kike duniani Februari 7,2023,
"Takwimu zinaonesha kuwa ukeketaji nchini bado ni tatizo hali inayotokana na baadhi ya jamii kuendelea kukumbatia mila na desturi zenye madhara na kuwadhalilisha watoto wa kike hivyo nitoe wito kwa Wanaume na Wavulana kote nchini kubadili mitizamo na kuongeza jitihada katika mapambano ya kupinga ukeketaji dhidi ya Wanawake na watoto wa kike," amesema Dkt.Gwajima
Dkt.Gwajima amesema kuwa maadhimisho hayo mwaka huu yatafanyika katika ngazi ya Mkoa kulingana na mazingira yao na kiwango cha hali ya ukeketeji katika mkoa husika ,hivyo Wakuu wa mikoa wana jukumu la kufanya maandalizi kuelekea siku hiyo.
Waziri huyo ameeleza kuwa madhara yanayotokana na ukeketaji ni pamoja na kupoteza damu nyingi ,kusababisha vifo, maambukizi ya VVU/UKIMWI na kusababisha matatizo wakati wa kujifungua.
Pia amesema kuwa watoto wakati wa kukeketwa hushindwa kuhudhuria shule kwenye vipindi kwa muda mrefu na hivyo kuzorotesha maendeleo yao kielimu.
"Serikali kwa kushirikiana na wadau inaendelea na jitihada za kukabiliana na vitendo vya ukeketaji kupitia mipango na mikakati iliwekwa ikiwemo kutunga na kufanya marekebisho ya sheria na sera mbalimbali za nchi,"
Na kuongeza kuwa "Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (1977) ,inasisitiza usawa na heshima kwa binadamu wote,kutambua na kuthamini utu wa mtu pamoja na kuhakikisha haki mbele ya sheria," amesema Dkt.Gwajima
Kwa upande wake Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Watoto Sehemu ya Familia Bi.Asha Shame amesema kuwa kwa sasa Tanzania ina asilimia 10 ya vitendo vya ukeketaji huku mikoa inayoongoza kwa vitendo hivyo ikiwa ni Manyara yenye asilimia 58,Dodoma ina asilimia 47,Arusha ina asilimia 41,Mara ina asilimia 32 na Singida ina asilimia 31.
Naye Mratibu wa Kutokomeza ukeketeaji Tanzania Bw.Denis Mose wakati akijibu swali kuhusu Mikoa inayoongoza kwa kuwa na wanaume wengi ambao hawajaingia tohara amesema kuwa baada ya kampeni iliyofanywa na Serikali kwa kushirikiana na mashiriki mbalimbali imesaidia mikoa ya Njombe,Iringa,Singida na Tabora Wanaume wengi kuingia katika vitendo hivyo vya tohara.
Februari 06, 2003 Baraza la Umoja wa Mataifa liliidhinisha kufanyika kwa Siku ya Kimataifa ya Kupinga Ukeketaji kwa Nchi Wanachama wa Umoja wa Mataifa kwa lengo la kutokomeza vitendo vya ukeketaji kwa wanawake na watoto wa kike duniani na Mwaka huu Maadhimisho hayo yatakwenda na kaulimbiu isemayo “Wanaume na Wavulana; Tushiriki Kupinga Mila na Desturi zenye Madhara ili kutokomeza Ukeketaji”.
No comments:
Post a Comment