NA. MWANDISHI WETU
Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi Mkoa wa Ruvuma, Oddo killian ameiasa jamii kuendelea kuchukua tahadhari za mapema katika kukabiliana na maafa badala ya kusubiri maafa kutokea.
Ametoa kauli hiyo wakati wa ziara ya Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu ayeshughulikia masuala yua Sera, Bunge na Uratibu Mhe Ummy Nderiananga alipotembelea ofisi za Chama cha Mapinduzi Mkoani humo ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kukagua utekelezaji wa hatua zinazochukuliwa kuzuia na kujiandaa kukabiliana na maafa kwa kamati ya usimamizi wa maafa katika mkoa huo.
Alieleza kuwa, ni wakati sasa kila mmoja kujua nafasi yake katika masuala ya menejimenti ya maafa nchini na kutosubiri Serikali na mamlaka zingine kuchukua hatua na kusema kuwa ni wajibu wa kila mmoja kuwa mzalendo katika jamii ili kuendelea kupunguza madhara yatokanayo na maafa nchini.
“Tuache tabia ya kusubiri matukio ndipo tuchukue hatua, kila mmoja kuanzia ngazi ya familia kuwe na mikakati madhubuti ya kukabiliana na maafa endapo yatatokea, hii inafanana na mtu anayejiandalia mazingira ya nyumba yake ya umilele anaweza kuonekana hafai ingawa tukiichukua hii kama mfano wa maandalizi yua kukabili maafa basi itatufaa hivyo tujiandae maadamu hatujui yaliyo mbele,” alisema
Aliongezea kuwa ipo haja ya elimu zaidi juu ya kukabiliana na masuala haya kuanzia ngazi za chini hadi mkoa ili wananchi waendelea kuchukua hatua katika kujiandaa, kukabiliana, kuzuia na kurejesha hali endapo maafa yanatokea.
Kwa upande wake Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Mhe Ummy Nderiananga aliupongea uongozi wa Chama cha Mapinduzi Mkoa wa Ruvuma kwa namna unavyoendelea kushirikiana na Serikali katika kuhakikisha masuala ya maendeleo hayarudi nyuma na kuwakumbusha kuendelea kuimarisha umoja huo katika kulijenga Taifa.
Akizungumzia ziara yake Naibu Waziri Ummy alisema Ofisi yake itaendelea kuzifikia Halmashauri zote kwa kutoa elimu kwa kuzingatia taarifa za utabiri zilizotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Nchini ili kujiandaa mapema kukabili maafa ya mvua za El nino.
Aidha alitumia nafasi hiyo kuwakumbusha viongozi wa chama hicho kuendelea kufanya kazi kwa bidii huku akiwaeleza kutokuwaacha nyuma watu wenye ulemavu katika masuala mbalimbali ikiwemo fursa zilizopo Mkoani humo.
No comments:
Post a Comment