
OR- TAMISEMI
Wanamichezo kutoka mikoa mbalimbali ya Tanzania wameendelea kuwasili mkoani Iringa kwa ajili ya kushiriki mashindano ya Umoja wa Michezo na Taaluma kwa Shule za Msingi (UMITASHUMTA) yanayotarajiwa kuanza rasmi tarehe 9 Juni, 2025.
Mashindano haya, pamoja na yale ya Umoja wa Michezo na Taaluma kwa Shule za Sekondari (UMISSETA), yanafanyika kitaifa katika Mkoa wa Iringa, na yanatarajiwa kufunguliwa rasmi na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Kassim Majaliwa.
Akizungumza mara baada ya kuwasili katika viwanja vya Shule ya Sekondari Iringa Wasichana, Afisa Elimu Msingi wa Halmashauri ya Ngara, Mwalimu James John Ling’wa, alisema Mkoa wa Kagera umejiandaa kikamilifu kushiriki katika mashindano ya mwaka huu.
“Tumejiandaa vizuri. Tumefika tukiwa na wanafunzi zaidi ya 100 na tuna uwakilishi wa kila mchezo. Tunamshukuru Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuipa michezo hii umuhimu mkubwa,” alisema Mwalimu Ling’wa.
Kwa upande wake, Kocha wa timu ya mpira wa miguu ya Mkoa wa Mwanza, Mainu David Kayombo, amesema wamewasili mapema Iringa ili kuwapa wachezaji muda wa kuzoea hali ya hewa na mazingira, ili waweze kushindana kwa ufanisi zaidi.
Mashindano ya UMITASHUMTA na UMISSETA 2025 yanaandaliwa na Ofisi ya Rais – TAMISEMI kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia pamoja na Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo.
Kaulimbiu ya mashindano ya mwaka huu ni:
"Viongozi bora ni msingi wa maendeleo ya Taaluma, Sanaa na Michezo. Shiriki Uchaguzi Mkuu 2025 kwa Amani na Utulivu."



No comments:
Post a Comment