Na Neema Mbuja, Nzega
Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia Sekta ya Mafuta na Gesi Wizara ya Nishati, Dkt James Mataragio, amesema utekelezaji wa mradi wa bomba la mafuta ghafi la Afrika Mashariki (EACOP) unazingatia maslahi mapana ya nchi ikiwemo upatikanaji wa ajira kwa wazawa, kuongezeka kwa pato la Taifa na ushirikishwaji wa kampuni za wazawa kutoa huduma kwenye utekelezaji wa mradi wa EACOP.
Dkt. Mataragio ameyasema hayo leo tarehe 28 Julai, 2025 wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya ziara yake ya kutembelea na kujionea maendeleo ya utekelezaji wa mradi wa EACOP hususani utekelezaji wa makubaliano kwenye mradi huo.
Akiwa kwenye kiwanda cha kuweka mifumo ya upashaji na utunzaji wa joto(Thermal Insulation System )Dkt.Mataragio alijionea namna mabomba yatakayotumika kusafirisha mafuta kutoka Hoima nchini Uganda hadi Chongoleani Tanga yanavyoandaliwa na kuwekwa teknolojia maalumu ya kudhibiti kutu eneo la Sojo wilaya ya Nzega mkoa wa Tabora.
‘’ Wizara ya Nishati ndio mwenye dhamana ya kusimamia maslahi ya Serikali chini ya TPDC na tumeridhika na maendeleo ya utekelezaji wa mradi kwa kuzingatia sheria na mikataba iliyopo, ambapo mpaka sasa fedha zote za mradi wa EACOP zimepatikana kwa asilimia mia moja’’ Amesema Dkt Mataragio
Ameongeza kuwa ujenzi wa bomba la mafuta ghafi la Afrika Mashariki unaendelea kwenye mikoa ya Kagera, Geita, Tabora,Singida,Dodoma,Manyara,na Tanga na utahusisha pia ujenzi wa vituo 4 vya kuongeza msukumo wa mafuta(Pump Stations) na vituo viwili vya kupunguza msukumo wa mafuta(Pressure reduction Stations) ambao umekamilika kwa asilimia 55
‘’ Ujenzi wa bomba la Mafuta ghafi la EACOP kwa sasa umefikia asilimia 65 na utagharimu kiasi cha Dola za kimarekani Bilioni 5.65 na jambo la kufurahisha ni kwamba ajira za wazawa takribani 9,194 zimezalishwa katika kipindi cha ujenzi wa mradi na kati ya hizo asilimia 75 zimenufaisha wazawa’’ Amesistiza Dkt Mataragio
Amesema mpaka sasa jumla ya shilingi bilioni 60 zimepatikana kutokana na manufaa ya utekelezaji wa mradi wa EACOP ikiwemo
Makusanyo ya pango la ardhi, ushuru wa huduma na usajili wa vibali mbalimbali kwenye halmashauri.
Ujenzi wa bomba la mafuta ghafi la Afrika Mashariki unatekelezwa na nchi mbili za Tanzania na Uganda ambapo kila moja ina hisa asilimia 15, ambapo UNOOC ya China asilimia 8 na Total Energies asilimia 62 ambapo mradi unatarajia kukamilika mwezi Julai, 2026.
No comments:
Post a Comment