Wizara ya ujenzi kupitia idara yake ya usalama na mazingira (DSE) imewataka wadau wa barabara
nchini kuzingatia utunzaji wa mazingira ili kuzilinda barabara zinazojengwa na kuzifanya eneo
salama kwa watumiaji.
Hayo yamesemwa na Eng. Joram Mduda wakati wa ziara ya ukaguzi wa barabara za NorangaItigi Km 25 mkoani Singida, na Mbulu-Garibab Km 25 mkoani Manyara zinazojengwa kwa
kiwango cha lami.
Katika ukaguzi huo wadau wa ujenzi wakiwemo wataalam kutoka Wakala wa barabara Tanzania
(TANROADS), wamekumbushwa masuala mbalimbali kuhusu kuzingatia usalama na mazingira
wanapojenga barabara.
Miongoni mwa maeneo yaliyokaguliwa ni kambi za wakandarasi na machimbo ya mawe na vifusi
vya kujengea barabara ambapo uchimbaji wa malighafi katika maeneo hayo unaendelea kuzingatia
taratibu za mazingira bila kusababisha athari kwa jamii.
Aidha, wataalam hao wamefanya tathmini ya utekelezaji wa mazingira na kutoa mafunzo ya
uhimilivu wa miundombinu ya barabara inayohusiana na tabianchi, sheria, muundo na majukumu
ya TANROADS.
Lengo la mafunzo hayo ni pamoja na kuleta athari chanya kwa wananchi na jamii kwa ujumla ili
kuhakikisha maeneo ya machimbo ya malighafi yanawekwa salama wakati na baada ya kumaliza
ujenzi wa mradi,pia kambi za wakandarasi kuhifadhi taka hatarishi zinazoweza kusababisha
madhara kwa wananchi waliopo karibu na ujenzi wa barabara.
Mafunzo hayo kwa wadau wa barabara na ufuatiliaji ni ya mara kwa mara ambapo yanalenga
kuhakikisha ujenzi wa miradi ya miundombinu ya barabara inatekelezwa kwa kuzingatia viwango
vya kitaalam vinavyopaswa kuzingatiwa ili kulinda mazingira na kuepusha changamoto
zinazoweza kuleta madhara kwa wananchi.




No comments:
Post a Comment