WADAU WA BARABARA MIKOA YA SINGIDA NA MANYARA WAFUNDWA - OKULY BLOG

Breaking

Music

Header ADS

Tuesday, February 24, 2026

WADAU WA BARABARA MIKOA YA SINGIDA NA MANYARA WAFUNDWA


Wizara ya ujenzi kupitia idara yake ya usalama na mazingira (DSE) imewataka wadau wa barabara
nchini kuzingatia utunzaji wa mazingira ili kuzilinda barabara zinazojengwa na kuzifanya eneo
salama kwa watumiaji.

Hayo yamesemwa na Eng. Joram Mduda wakati wa ziara ya ukaguzi wa barabara za NorangaItigi Km 25 mkoani Singida, na Mbulu-Garibab Km 25 mkoani Manyara zinazojengwa kwa 
kiwango cha lami.

Katika ukaguzi huo wadau wa ujenzi wakiwemo wataalam kutoka Wakala wa barabara Tanzania 
(TANROADS), wamekumbushwa masuala mbalimbali kuhusu kuzingatia usalama na mazingira 
wanapojenga barabara.

Miongoni mwa maeneo yaliyokaguliwa ni kambi za wakandarasi na machimbo ya mawe na vifusi 
vya kujengea barabara ambapo uchimbaji wa malighafi katika maeneo hayo unaendelea kuzingatia 
taratibu za mazingira bila kusababisha athari kwa jamii.

Aidha, wataalam hao wamefanya tathmini ya utekelezaji wa mazingira na kutoa mafunzo ya 
uhimilivu wa miundombinu ya barabara inayohusiana na tabianchi, sheria, muundo na majukumu 
ya TANROADS.

Lengo la mafunzo hayo ni pamoja na kuleta athari chanya kwa wananchi na jamii kwa ujumla ili 
kuhakikisha maeneo ya machimbo ya malighafi yanawekwa salama wakati na baada ya kumaliza 
ujenzi wa mradi,pia kambi za wakandarasi kuhifadhi taka hatarishi zinazoweza kusababisha 
madhara kwa wananchi waliopo karibu na ujenzi wa barabara.

Mafunzo hayo kwa wadau wa barabara na ufuatiliaji ni ya mara kwa mara ambapo yanalenga 
kuhakikisha ujenzi wa miradi ya miundombinu ya barabara inatekelezwa kwa kuzingatia viwango 
vya kitaalam vinavyopaswa kuzingatiwa ili kulinda mazingira na kuepusha changamoto 
zinazoweza kuleta madhara kwa wananchi.

No comments:

Post a Comment