***************
Na. James K. Mwanamyoto-Bagamoyo
Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi amesema ameridhishwa na namna walengwa wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini wa Kijiji cha Nia Njema wilayani Bagamoyo walivyoboresha maisha yao kupitia ruzuku inayotolewa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF).
Mhe. Mhe. Ndejembi amesema hayo leo wakati akizungumza na Walengwa wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini wa Kijiji cha Nia Njema wilayani Bagamoyo wakati wa ziara yake ya kikazi iliyolenga kukagua utelekezaji wa mpango huo wilayani humo.
Mhe. Ndejembi amesema mafanikio waliyoyapata walengwa hao kwa kujishughulisha na masuala mbalimbali ya ujasiriamali ikiwemo ushonaji wa nguo, ususi wa mikeka, vikapu, ufugaji wa kuku na kilimo yanaendana na lengo la Serikali la kuinua uchumi wa wananchi wake kupitia TASAF.
“Mafanikio mliyoyapata kupitia TASAF yanafurahisha sana na yanampa nguvu Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan ya kuendelea kuiwezesha TASAF ili wananchi wengi waendelee kunufaika na kuboresha maisha yao,” Mhe. Ndejembi ameongeza.
Aidha, Mhe. Ndejembi amewataka walengwa wa TASAF kushiriki zoezi la Sensa ya Watu na Makazi litakayofanyika tarehe 23 Agosti, 2022 ili kuiwezesha Serikali kupanga mipango ya maendeleo ikiwemo ya miradi inayotekelezwa na TASAF.
Mhe. Ndejembi ameongeza kuwa, walengwa wa TASAF wanatakiwa kuwa mstari wa mbele kutoa elimu kwa wengine kushiriki zoezi la Sensa ili Serikali ipate idadi kamili ya watu na kupanga mipango yake ya maendeleo.
Akizungumzia namna TASAF ilivyoboresha maisha yake, mmoja wa walengwa wa TASAF, Bibi Elizabeth Stephen ameishuru Serikali kwa kumpatia ruzuku inayomuwezesha kulea watoto wake wawili wenye ulemavu, kufuga kuku na kufungua genge ambalo linamuingiza kipato kinachoendesha maisha yake.
No comments:
Post a Comment