Na Okuly Julius-Dodoma
Naibu Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhandisi Mathew Kundo amevitaka vyombo vya habari kuanzisha vipindi vinavyo hamasisha mila na Destiri ya mtanzania ili kuwaelimisha vijana kuhusu tamaduni zao.
Mhandisi Kundo ametoa kauli hiyo Leo Februari 13,2024 Jijini Dodoma , alipomuwakilisha Waziri wa Habari Mhe. Nape Nnauye, katika ufunguzi wa Mkutano wa Mwaka wa Vyombo vya Utangazaji Nchini ulioenda sambamba na kilele cha maadhimisho ya siku ya Utangazaji Duniani
“Ni muhimu sana kwenu TCRA kuliangalia suala hili kwa umakini mkubwa kwani Mkifanya hivi itawasaidia sana kufanya kazi kwa ufanisi,na Sisi kama Serikali tunawaahidi kuendeleza ushirikiano uliopo ili kuleta maendeleo kwa jamii, "amesema Mhandisi Kundo
Pia Mhandisi Kundo ameiagiza Mamlaka ya Mawasiliano nchini (TCRA),kuhakikisha inajitathmini Mara kwa Mara ili kujua ni wapi kuna mapungufu na kuweza kuyafanyia kazi mapungufu hayo.
Katika hatua nyingine Mhandisi Kundo amebainisha kuwa katika kuelekea uchaguzi wa Serikali za Mitaa Vyombo vya Habari vinatakiwa kuwa mstari wa mbele katika kuzingatia Maadili na kanuni za utoaji Habari kwa jamii kwa maslahi ya Taifa.
“Vyombo vya habari vina wajibu mkubwa katika Taifa letu hivyo Ni muhimu kila mmoja kuzingatia taaluma na kutimiza majukumu yake kwa weledi mkubwa,amesisitiza Naibu Waziri
Aidha amewaasa Waandishi wa habari kuhakikisha wanazingatia usawa katika kuripoti matukio ya kampeni za Uchaguzi na matokeo Yake bila upendeleo
Kwa upande Wake Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania( TCRA )Jones Kilimbe amewataka watangazaji na waandishi wa habari kuzingatia Madili na kanuni ya kazi zao.
Amegusia pia uchaguzi ujao wa Serikali za mitaa kuwa,vyombo vya habari vina jukumu la kutoa elimu kwa wapiga kura ikiwa ni pamoja na kuhabarisha umma kuhusu mwenendo mzima wa kampeni bila upendeleo na kutoa ripoti sahihi za siku ya kupiga kura.
Amesema TCRA kama wadau wa Utangazaji watahakikisha wanakuwa bega kwa bega na vyombo vya Utangazaji kwa kuhakikisha wanatoa mwelekeo wa maudhui yenye ubora bila upotoshaji.
"Maudhui ya Utangazaji ni chakula kwa jamii, yanaweza kujenga au kubomoa, kuharakisha maendeleo au kukwamisha hivyo ni jukumu la vyombo vya Utangazaji kujikita katika kuhabarisha umma maeneo yenye tija na kuachana na uchochezi au uvunjifu wa Madili, " amesema
Naye Mwenyekiti wa wamiliki wa Vyombo vya Habari Nchini( MOAT)Samwel Nyala amesema pamoja na kukuza tasnia ya habari bado kuna changamoto mbalimbali ikiwemo gharama kubwa ya leseni hali inayowakwambisha na kuwapa hasara ya uendeshaji .
Kutokana na hali hiyo ameiomba Serikali kuangalia suala hilo ikiwa ni pamoja na kuangalia suala la ruzuku kwa Vyombo vya Habari kutokana na kuwepo kwa mdororo wa Uchumi.
Kwa upande wake mdau wa habari kutoka Chama cha watangazaji (NIPA) Amos Ngosha ameeleza masikitiko yake kuhusu hali ya uchumi wa vyombo vya habari kuwa imedorora kutokana na kukosa ruzuku kutoka Serikalini.
Ametumia nafasi hiyo kuiomba Serikali kuanza kutoa ruzuku kwa vyombo vya habari ili viweze kujiendesha.
"Tunashindwa kujiendesha kwa kukosa matangazo, matangazo yetu yamekuwa ni ya waganga wa tiba asili na viongozi wa dini,tunatozwa Kodi kubwa kuliko faida tunayoipata, tunaomba taaluma hii iheshimiwe kwa kutupunguzia gharama za uendeshaji, " amesema
No comments:
Post a Comment