
Halmashauri Kuu ya Utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Kilombero Mkoani Morogoro imeipongeza Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kwa kufikisha umeme katika Vijijini vyote 110 vya Wilaya hiyo pamoja na Vitongoji 283 kati ya 458.
Pongezi hizo zimetolewa leo na Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Kilombero, Mohamed Msuya wakati wa uwasilishwaji wa taarifa ya utekelezaji wa Ilani ya CCM ya 2020-2025 huku akiwapongeza Madiwani, Wabunge na Watendaji wa Serikali.
“Tuwapongeze sana Waheshimiwa Madiwani, Wabunge kwa kusimamia Ilani ya CCM katika Wilaya yetu kufanikiwa. Lakini pia tuwapongeze sana Watendaji wa Serikali kwa kusimamia maelekezo ya ilani,” amepongeza Mwenyekiti huyo.
Awali akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa Ilani ya CCM kwa Wajumbe wa Mkutano huo, Mkuu wa Wilaya ya Kilombero, Mhe. Dunstan Kyobya amempongeza na kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha zilizowezesha kutekelezwa kwa miradi iliyoahidiwa katika Ilani ya CCM katika Wilaya hiyo.
Kwa upande wake, Meneja wa Miradi kutoka REA, Mhandisi Romanus Lwena ameahidi kuwa Wakala utaendelea kufanya kazi usiku na mchana kuhakikisha vitongoji ambavyo bado havijafikiwa na umeme vinapata umeme ili lengo la Serikali la kuendelea kuboresha maisha ya Watanzania linatimia.











No comments:
Post a Comment