VIONGOZI WA KIMASAI WAAHIRISHA TOHARA KWA VIJANA 2, 000 KUPISHA UCHAGUZI MKUU - OKULY BLOG

Breaking

Music

Header ADS

Friday, October 17, 2025

VIONGOZI WA KIMASAI WAAHIRISHA TOHARA KWA VIJANA 2, 000 KUPISHA UCHAGUZI MKUU


Laigwanani Mkuu wa Jamii ya Kimasai nchini Tanzania Bwana Isack Ole Kisongo Meijo ametangaza kusogezwa mbele kwa zoezi la tohara kwa Vijana wa kimasai lililokuwa lifanyike kuanzia Oktoba 21-30 mwaka huu ili kutoa fursa kwa Vijana zaidi ya 2, 000 waliokuwa washiriki kwenye zoezi hilo kwenda kushiriki kupiga kura Oktoba 29, 2025.

Ole Kisongo ametoa maelezo hayo leo oktoba 17, 2025 mbele ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mhe. CPA Amos Gabriel Makalla wakati wa Baraza la Maigwanani Mkoa wa Arusha, akimuhakikishia Mkuu wa Mkoa kuwa wapo tayari kwa uchaguzi na kulinda kulinda amani wakati wote wa uchaguzi Mkuu kwenye jamii yao.

"Hiyo siku ni takatifu katika Taifa la Tanzania, Hiyo siku ni njema na tumeambiana jamii ya kimasai kuwa hatujawahi kushika mkia, tunataka kujitokeza kwa wingi kupiga kura katika Vijiji vyetu sasa Ukitahiri Vijana 1,000 leo utapunguza kura kwani Mgonjwa atashindwa kwenda kupiga kura. Tunataka kushiriki vyema kupiga kura sote." Amesisitiza Ole Kisongo.

Kwa upande wake Mhe. Makalla katika salamu zake amewapongeza na kuwashukuru Viongozi na Jamii nzima ya Kimasai kwa kutambua umuhimu wa amani na kuridhika na kazi nzuri ya kimaendeleo inayoendelea kutendwa na serikali ya awamu ya sita, akiwahamasisha kuwa mabalozi wazuri wa kuhamasisha wengine kujitokeza kupiga kura na kulinda amani ya nchi.

CPA Makalla pia amewataka wananchi mara baada ya kupiga kura kurejea majumbani mwao na kuachia mamlaka husika kuendelea na zoezi la usimamizi na ulinzi wa kura, akiwahakikishia kuwa Vyombo vya ulinzi na usalama vimejipanga kikamilifu kuhakikisha Mkoa unakuwa salama na tulivu kuanzia sasa, wakati wa kura na baada ya uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025.

No comments:

Post a Comment