MHE. LIJUALIKALI ATOA NENO KWA KAMATI ELEKEZI YA WILAYA YA USIMAMIZI WA MAAFA - OKULY BLOG

Breaking

Music

Header ADS

Tuesday, January 20, 2026

MHE. LIJUALIKALI ATOA NENO KWA KAMATI ELEKEZI YA WILAYA YA USIMAMIZI WA MAAFA


NA. MWANDISHI WETU - NKASI


Mkuu wa Wilaya ya Nkasi, Mheshimiwa Peter Lijualikali amepongeza Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu kwa namna ilivyoratibu zoezi la uandaaji wa Rasimu za Nyaraka za Usimamizi wa Maafa kwa Wilaya yake huku akiwasihi wajumbe wa kamati kuzitumia kama ilivyokusudiwa mara baada ya uzinduzi utakaofanyika hivi karibuni.

Ameyasema hayo leo tarehe 20 Januari, 2026 wakati wa kikao cha Kamati Elekezi ya Wilaya ya Usimamizi wa Maafa ikihudhuriwa na timu ya wajumbe hao wakiongozwa na mkuu wa Wilaya huyo ambaye ndiye Mwenyekiti wa Kamati.

“Kipekee nawapongea Ofisi ya Waziri Mkuu na UNICEF kwa kuona umuhimu wa kuja katika Wilaya yetu ya Nkasi, na tutahakikisha kile mlichokifanya hapa Nkasi kinaleta matokeo chanya hasa kwa elimu tuliyoipata ya masuala ya usimamizi wa maafa hususani katika kuzuia na kujiandaa ili kusiwe na athari kubwa endapo majanga yatatokea,” alieleza Mhe. Lijualikali.

Naye Mratibu wa Maafa Mkoa wa Rukwa Bi. Aziza Kalyatila amesema ipo haja ya kuendelea kupewa elimu zaidi ya masuala ya usimamizi wa maafa kwani itasaidia katika kuwajengea uwezo wa kuzuia, kujiandaa, kukabili, na kurejesha hali pindi maafa yanapotokea.

Kikao hicho kimeandaliwa na Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu kwa kushirikiana na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF) pamoja na timu ya wataalamu kutoka ofisi ya Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi kikilenga kuwapitisha katika nyaraka zilizoandaliwa kwa ajili ya matumizi ya Halmashauri ambazo ni Tathmini ya Vihatarishi vya Majanga, Uwezekano wa Kuathirika na Uwezo wa Kukabiliana na Majanga, rasimu ya Mpango wa Kujiandaa na Kukabiliana na Maafa pamoja na rasimu ya Mkakati wa kupunguza vihatarishi vya maafa.

No comments:

Post a Comment