
Na Okuly Julius, OKULY BLOG - DODOMA
Mkuu wa Chuo cha Uhasibu Arusha (IAA), Prof. Eliamani Sedoyeka, amesema changamoto kubwa inayowakabili vijana wengi nchini katika safari ya kujiajiri ni ukosefu wa elimu ya fedha na elimu ya rasilimaliwatu.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma, Prof. Sedoyeka amesema vijana wengi wana ujuzi wa kitaaluma na kiufundi, lakini wanakosa maarifa ya namna ya kuugeuza ujuzi huo kuwa fursa ya ajira binafsi na chanzo cha kuajiri wengine.
“Vijana wana ujuzi, lakini changamoto imebaki katika namna ya kubadilisha ujuzi huo kuwa ajira kwa kujiajiri wenyewe na hatimaye kuajiri wengine,” amesema Prof. Sedoyeka.
Katika hatua nyingine, amesema IAA ni miongoni mwa taasisi za umma zilizonufaika na Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi (HEET), unaofadhiliwa kwa mkopo wa masharti nafuu kutoka World Bank kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia chini ya Serikali ya Awamu ya Sita.
Amesema chuo hicho kimepata Shilingi 48,469,498,473/= kupitia mradi huo kwa ajili ya kuboresha miundombinu, kuendeleza mitaala na kuongeza fursa kwa vijana nchini.
Kwa mujibu wa Prof. Sedoyeka, fedha hizo zimeelekezwa katika maeneo ya kipaumbele ikiwemo ujenzi na uboreshaji wa miundombinu ya kufundishia na kujifunzia, mapitio ya mitaala ili iendane na mahitaji ya soko la ajira, kuimarisha matumizi ya teknolojia na TEHAMA, pamoja na kuwajengea uwezo watumishi wa chuo.
Katika kuimarisha uhusiano kati ya chuo na sekta ya ajira, IAA imeunda Kamati ya Ushauri ya Kisekta (Industrial Advisory Committee) itakayosaidia kutoa ushauri katika maandalizi na mapitio ya mitaala ili kuhakikisha wahitimu wanapata ujuzi unaohitajika katika mazingira halisi ya kazi.
Aidha, chuo hicho kimesaini jumla ya Hati za Makubaliano ya Ushirikiano (MoUs) 23 na taasisi mbalimbali za umma na binafsi, ikiwemo CEOs Round Table, kwa lengo la kuwapatia wanafunzi fursa za mafunzo kwa vitendo (internship), mafunzo ya vitendo kazini (field attachment), pamoja na kushiriki tafiti zinazolenga kutatua changamoto halisi za biashara na uchumi.
Kwa upande wa maboresho ya mitaala, Prof. Sedoyeka amesema IAA imekamilisha mapitio ya mitaala 15 kwa gharama ya takribani Shilingi milioni 160, huku Shilingi 446,000,000/= zikitengwa kwa ajili ya mapitio na utengenezaji wa mitaala mipya. Mitaala iliyofanyiwa mapitio ni pamoja na Sayansi ya Kompyuta, TEHAMA, Benki, Bima, Fedha na Mikopo.
Amesema mapitio hayo yamekidhi matakwa ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na kuthibitishwa na Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTVET).
Katika hatua nyingine, kupitia HEET, IAA imeanza utengenezaji wa mitaala mipya mitano katika kampasi za Babati na Songea. Katika Kampasi ya Babati, mitaala miwili imebuniwa katika fani za Uhandisi – Uchomeleaji na Teknolojia za Usindikaji wa Vyakula. Nayo Kampasi ya Songea imebuni mitaala mitatu katika fani za Usimamizi wa Biashara za Misitu, Usimamizi wa Biashara katika Mazao ya Maziwa na Usimamizi wa Biashara katika Uvuvi.
Sambamba na hilo, mradi huo unatarajiwa kufadhili ujenzi wa maabara za kisasa na karakana katika kampasi hizo, pamoja na programu za kuwajengea uwezo walimu na wataalamu katika nyanja husika.
Prof. Sedoyeka ameongeza kuwa utekelezaji wa mitaala hiyo unategemea uwepo wa wahadhiri mahiri, ambapo kupitia HEET, wahadhiri 115 wanaendelea na masomo ya Shahada ya Uzamivu (PhD) katika vyuo mbalimbali ndani na nje ya nchi.
Amesisitiza kuwa maboresho hayo yanalenga kuhakikisha IAA inaandaa wahitimu wenye ujuzi, ubunifu na uwezo wa kushindana katika soko la ajira la ndani na kimataifa, huku wakichangia kwa vitendo katika mageuzi ya kiuchumi ya taifa.

No comments:
Post a Comment