
Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Hamza S. Johari amewataka Watumishi wa Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria kufanya kazi kwa Weledi na Ufanisi ili kufikia malengo ya Ofisi kwani ana Imani kubwa na utendaji kazi wa OFISI ya Mwandishi Mkuu wa Sheria.
Mhe. Johari amesema hayo alipofungua kikao cha kwanza cha Baraza la Wafanyakazi la Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria tarehe 6 Machi, 2026 jijini Dar es Salaam.

*"Niwaombe muendelee kutekeleza majukumu ya Ofisi hii kwa Weledi na Ufanisi ili kufikia malengo ya Ofisi na nina imani kubwa na utendaji kazi wa Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria”* amesema Mhe. Johari
Aidha Mhe. Johari ameendelea kwa kuwataka watumishi wa Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria kuzingatia kanuni na Sheria za Utumishi wa Umma ili kutoathiri utendaji kazi wa Serikali.

*"Utumishi wa Umma unaongozwa na Sheria pamoja na Kanuni, hivyo natoa rai kwa watumishi wote tuzingatie Miongozo ya Utumishi wa Umma ili tusiathiri utendaji kazi wa Serikali,"* ameongeza Mhe. Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
Vilevile Mhe. Johari ameitaka Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria kuboresha matumizi ya mifumo ya TEHAMA ili kufanya kazi kwa ufanisi zaidi.
*"Naomba nisisitize matumizi ya mifumo ya TEHAMA ili kurahisisha utendaji kazi na kutoa kazi zenye ufanisi kwa matumizi ya Serikali na jamii kwa ujumla,"* ameeleza Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. Hamza Johari.

Awali, akimkaribisha Mgeni Rasmi, Mwandishi Mkuu wa Sheria, Bw. Onorius Njole, amesema Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria imewekeza nguvu kubwa kwenye mifumo ya TEHAMA ili kuendelea kuimarisha utendaji kazi.
*"Katika kuendelea kuimarisha utekelezaji wa Uandishi wa Sheria tumeamua kuweka nguvu kubwa kwenye mifumo ya Tehama kwa kuanzisha e-drafting, e-translation na e-revision na kwa usaidizi wako Mwanasheria Mkuu wa Serikali tutaweza kufanikisha hili.* amesema.
Pia, Mwandishi Mkuu wa Sheria Bw. Njole amemshukuru Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kuendelea kuwa kiongozi bora na mwenye msaada mkubwa kwa Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria.
*"Kwa niaba ya menejimenti ya Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria na Wafanyakazi wote, tunamshukuru Sana Mhe. Johari kwa kuwa kiongozi bora kwa Ofisi yetu, na kutupa ushirikiano kila tunapohitaji”* Amesema.
Miongoni mwa Wageni waalikwa katika Baraza la Wafanyakazi wa Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria ni Mkurugenzi wa Mashtaka, Bw. Sylvester Mwakitalu
Baraza la kwanza la Wafanyakazi wa Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria, limefanyika tarehe 6 Machi, 2026 katika ukumbi wa Mikutano wa Julius Nyerere (JNICC) jijini, Dar es salaam.

No comments:
Post a Comment