VIJANA WAASWA KUTUMIA MIKOPO NAFUU - OKULY BLOG

Breaking

Music

Header ADS

Thursday, May 21, 2026

VIJANA WAASWA KUTUMIA MIKOPO NAFUU


Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb), akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Dkt. Neema Majule, aliyetaka kujua wakati ambao Serikali itawasaidia wahitimu wa vyuo kutumia vyeti vyao kama dhamana kupata mikopo ya kuanzisha miradi ya uwekezaji, bungeni jijini Dodoma.

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Fedha)


Na. Jordan Mbwambo, WF, Dodoma


Serikali imewataka vijana wanaohitimu vyuo kutumia fursa zilizopo kupitia mifuko na programu mbalimbali zinazosimamiwa na Serikali ikiwemo Mfuko wa Vijana, ambayo hutoa mikopo yenye riba nafuu, ili kuwawezesha kuanzisha na kuendeleza shughuli zao za kiuchumi.

Hayo yamebainishwa bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb), alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Dkt. Neema Peter Majule, aliyetaka kujua wakati ambao Serikali itawasaidia wahitimu wa vyuo kutumia vyeti vyao kama dhamana kupata mikopo ya kuanzisha miradi ya uwekezaji.

Mhe. Luswetula, alisema kuwa Serikali ipo katika hatua za mwisho za kuandaa Sheria ya Dhamana kwa mali zinazohamishika, yenye lengo la kutambua rasmi mali hizo kama dhamana katika utoaji wa mikopo.

“Benki Kuu ya Tanzania ili kuimarisha usimamizi, uwazi na ufuatiliaji wake, miongoni mwa mali zinazopendekezwa kufanyiwa tathmini ni vyeti vya taaluma vya wahitimu wa vyuo kwa lengo la kuchunguza uwezekano wa kuvifanya vitumike kama dhamana katika upatikanaji wa mikopo”, alifafanua Mhe. Luswetula.

Aliongeza kuwa benki na taasisi za fedha hutumia aina mbalimbali za dhamana katika utoaji wa mikopo kwa watu binafsi, kwa mujibu wa Sheria ya Ardhi, Sura ya 113 ambapo dhamana inayotambuliwa kwa kiwango kikubwa ni ile inayohusiana na mali zisizohamishika hususan ardhi na majengo.

No comments:

Post a Comment