Na Mwandishi Wetu, Njombe
MKOA wa Njombe unatarajiwa kuwa kitovu kipya cha uchumi wa madini nchini kufuatia uwekezaji mkubwa katika miradi ya uchimbaji na uchakataji wa madini ya chuma inayolenga kufungua maelfu ya ajira, kukuza biashara za ndani na kuongeza mapato kwa wananchi wa Wilaya ya Ludewa.
Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Njombe, Mhandisi Lucas Mlekwa, amesema tayari moja ya miradi mikubwa inayosimamiwa na Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC) kwa kushirikiana na kampuni ya kigeni imepata Leseni Kubwa ya Uchimbaji wa Madini baada ya utafiti wa kina uliofanyika kati ya mwaka 2012 na 2013 kubaini uwepo wa zaidi ya tani milioni 126 za madini ya chuma.
Amesema tafiti hizo pia zimeonesha uwepo wa madini mengine yenye thamani kubwa yanayoambatana na chuma ikiwemo titanium na vanadium, hatua inayoongeza thamani ya kiuchumi ya mradi huo kwa Taifa.
“Kwa sasa tupo katika hatua za mwisho za kukamilisha makubaliano kati ya Serikali na wawekezaji, na tunatarajia ndani ya mwaka mmoja utekelezaji rasmi wa mradi utaanza,” amesema Mlekwa.
Kwa mujibu wa Mlekwa, mradi huo utahusisha shughuli kuu mbili ambazo ni uchimbaji wa madini pamoja na ujenzi wa kiwanda cha kisasa cha kuchakata chuma kitakachozalisha bidhaa mbalimbali zitakazotumika katika sekta ya ujenzi na viwanda nchini.
Ameeleza kuwa utekelezaji wa miradi hiyo utaongeza ushiriki wa wazawa kupitia utekelezaji wa sera ya Ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini, ambapo wananchi watanufaika na fursa za ajira na biashara zikiwemo huduma za ulinzi, usafirishaji, ugavi wa vifaa vya ujenzi, huduma za migodini pamoja na shughuli nyingine za kiuchumi zinazozunguka miradi hiyo.
Aidha, amesema mradi wa chuma wa Maganga Matitu unaosimamiwa pia na NDC kwa ubia na kampuni ya kigeni umefikia hatua za mwisho za maandalizi baada ya mwekezaji kulipa zaidi ya Shilingi bilioni 4.2 kama fidia kwa wananchi waliopisha eneo la mradi huo, ambao una akiba inayokadiriwa kufikia tani milioni 45 za madini ya chuma.
Mlekwa ameongeza kuwa pamoja na miradi hiyo, Wilaya ya Ludewa itanufaika na utekelezaji wa mradi wa Mchuchuma wenye zaidi ya tani milioni 428 za makaa ya mawe kwa ajili ya uzalishaji wa umeme, unaotarajiwa kuimarisha upatikanaji wa nishati kwa shughuli za uchimbaji na viwanda vya chuma vitakavyojengwa wilayani Ludewa.
Amesema maendeleo hayo yataifanya Njombe kuwa miongoni mwa maeneo muhimu zaidi nchini katika sekta za madini, viwanda na nishati, huku yakitarajiwa kuongeza mchango wa sekta ya madini katika ukuaji wa uchumi wa Taifa na maendeleo ya wananchi wa eneo hilo.




No comments:
Post a Comment