Seoul, Korea,
Ubalozi wa Tanzania nchini Korea Kusini kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa
Dodoma imeendesha Jukwaa la Biashara na Uwekezaji (Trade and Investment Forum)
lililokuwa na kaulimbiu ya Kuonesha Fursa lukuki zilizopo Mkoani Dodoma.
Jukwaa hilo
lilihusisha zaidi ya Wawekezaji na Wafanyabiashara wakubwa 60, hususan kutoka katika jiji
la kibiashara la Seoul.
Jukwaa hilo lililenga kutangaza fursa za uwekezaji zilizopo Mkoani Dodoma na kuvutia
wawekezaji katika sekta za Kilimo, Utalii na Ukarimu, Uchukuzi na Usafirishaji.
Vilevile
sekta za Viwanda na Biashara, Uchimbaji wa Madini, Huduma za maji, Usafi wa mazingira
na Ujenzi wa Majengo na Miundombinu (Real estate).
Mgeni rasmi kwenye tukio hilo alikuwa ni Mhe. Dkt Ramadhani Rajabu Seif, Naibu Waziri,
Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa. Katika hotuba yake
Mheshimiwa Naibu Waziri aliyakaribisha makampuni yaliyoshiriki kwenye Jukwaa hilo
kuwekeza nchini Tanzania hususan, katika mkoa wa Dodoma, akiwahakikishia ushirikiano
mkubwa kutoka serikalini.
“Tanzania ni nchi yenye utulivu na amani, mazingira mazuri na salama ya biashara na
uwekezaji, hivyo tunawakaribisha sana kuwekeza katika nchi yetu,” alisema Mheshimiwa
Seif.
Naye Balozi wa Tanzania nchini Korea Kusini Mheshimiwa. Noel Kaganda aliwashukuru
washiriki wa Jukwaa hilo kwa kukubali mwaliko na kujitokeza kwa wingi.
Aidha
aliwahakikishia wawekezaji kuwa Ubalozi utaendelea kutoa ushirikiano na taarifa za kutosha
kuhusu fursa za biashara na uwekezaji zilizopo ncini Tanzania ikiwemo katika Mkoa wa
Dodoma, Mji Mkuu wa Tanzania.
Hali kadhalika Mheshimiwa. Rosemary Staki Senyamule, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma
alifafanua kuhusu fursa mbalimbali za uwekezaji zilizopo mkoani Dodoma kama vile kilimo
cha Zabibu, Ufuta, Alizeti, Tufaa na Korosho. Pia alisisitiza juu ya vivutio mbalimbali
vilivyopo mkoani Dodoma ukiwemo Utalii katika mbuga za Mkungunero na Swagaswaga;
Utalii wa kihistoria hususan michoro ya miambani iliyopo Kondoa Irangi, utalii wa
utamaduni; utalii wa mikutano; na michezo.
Vilevile, Mheshimiwa Senyamule alizungumzia fursa za uwekezaji katika sekta za uchukuzi
na usafirishaji, hususan ujenzi wa reli za mijini kwa ajili ya kurahisisha usafiri katika jiji la
Dodoma.
“Mkoa wa wetu unahitaji huduma hizi kwa sasa ili kuongeza kasi ya maendeleo kwa wakazi
wa Dodoma, ambapo ongezeko la watu linazidi kukua kwa kasi kubwa,” Alisema.
Pia Mkuu wa Mkoa alisisitiza uwepo wa fursa za biashara na uwekezaji katika sekta za
viwanda na madini, ambapo mkoa wa Dodoma una zaidi ya aina 49 za madini adimu na ya
kimkakati.
Kongamano lilikuwa na mawasilisho sita; ambapo mawasilisho matatu yalitoka Tanzania
yakihusisha fursa za biashara na uwekezaji, mradi wa ujenzi wa Mji wa Kisasa wa Hombolo
(Hombolo Thematic Satellite City) na mradi wa ujenzi wa reli za mjini. Kwa upande wa Korea
Kusini kulikuwa na mawasilisho matatu juu ya uzoefu wa uwekezaji wa Korea nchini
Tanzania, na mazingira ya uwekezaji nchini.
Wazungumzaji wa Makampuni hayo walikuwa
ni: - Mtendaji Mkuu wa kampuni ya KFINCO, Mwenyekiti na Mtendaji mkuu wa Kmapuni
ya KOIMA, Mwenyekiti wa Kampuni ya ICAK, Waziri wa Ardhi, Miundombinu na
Uchukuzi (Mstaafu).
Makampuni aliyotoa uzoefu ni KORAIL, HEELIM na Mwenyekiti wa
Chama cha Wafanyabiashara wa Korea nchini Tanzania.
UBALOZI WA TANZANIA NCHINI KOREA
SEOUL





No comments:
Post a Comment