JARIBIO LA KWANZA LA VIAZI MVIRINGO DODOMA LAONESHA MAFANIKIO MAKUBWA - OKULY BLOG

Breaking

Music

Header ADS

Wednesday, August 12, 2026

JARIBIO LA KWANZA LA VIAZI MVIRINGO DODOMA LAONESHA MAFANIKIO MAKUBWA



Na Mwandishi Wetu – DODOMA RS


Jaribio la kwanza la mbegu mpya ya viazi mviringo iliyofanyiwa utafiti na Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI) limeonesha mafanikio makubwa katika Mkoa wa Dodoma, baada ya zao hilo kustawi katika shamba la Makamu wa Rais Mstaafu, Mhe. Dkt. Philip Mpango, lililopo Kijiji cha Mayamaya, Wilaya ya Bahi.

Jaribio hilo lililodumu kwa siku 104, kuanzia upandaji hadi uvunaji, limeonesha kuwa viazi mviringo vinaweza kustawi katika mazingira ya Dodoma, hivyo kufungua fursa mpya ya uzalishaji wa chakula na kuongeza kipato kwa wakulima.

Akizungumzia matokeo ya jaribio hilo, Mhe. Dkt. Philip Mpango ameishukuru TARI kwa kusimamia utafiti huo na kusema mafanikio yaliyopatikana Mayamaya ni hatua muhimu katika kuonesha uwezekano wa kuongeza wigo wa mazao yanayolimwa mkoani Dodoma.

Amewahimiza wakazi wa Dodoma kuchangamkia fursa hiyo mara baada ya utafiti kukamilika na mbegu husika kuthibitishwa kwa matumizi ya kibiashara.

“Wakazi wa Dodoma sasa tuanze kuchangamkia hii fursa. TARI wako tayari kutusaidia kwa kutupatia mbegu bora zinazofaa zaidi. Hii itatusaidia kupata chakula na kipato kwa ajili ya kusaidia watoto wetu kwenda shule. Dodoma si nusu jangwa; ni suala la kupata maarifa ya kuvuna na kuhifadhi maji kwa ajili ya kuendeleza kilimo chetu. Hatuwezi kuendelea kutegemea mtama, mahindi, zabibu au alizeti pekee; lazima tuongeze mazao mengine,” amesema Mhe. Dkt. Mpango.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa TARI, Dkt. Thomas Bwana, amemshukuru Mhe. Dkt. Mpango kwa kuruhusu taasisi hiyo kufanya jaribio katika shamba lake na kueleza kuwa TARI inapanga kuendeleza majaribio ya zao hilo kwa wakulima wadogo wanaotegemea kilimo cha mvua.

Dkt. Bwana amesema TARI itaendelea kufanya tafiti za mazao mbalimbali katika maeneo tofauti Nchini, ili kuondoa dhana kwamba maeneo fulani yanafaa kwa mazao maalumu pekee. Pia amewahimiza wananchi, hususan wakulima, kuendelea kushirikiana na TARI kwa kuruhusu tafiti na majaribio ya kilimo kufanyika katika mashamba yao.

Kwa mujibu wa Mtafiti Kiongozi wa zao la viazi mviringo kutoka Kituo cha TARI Uyole, Dkt. Owekisha Kwigizila, mbegu hiyo mpya ina uwezo wa kukomaa ndani ya takribani siku 90, kustahimili ukame na baadhi ya magonjwa, huku ikiwa na uwezo wa kuzalisha kati ya tani 35 hadi 40 kwa hekta moja.

Baadhi ya wakazi wa Kijiji cha Mayamaya walioshiriki katika zoezi la uvunaji wameeleza kufurahishwa na namna zao hilo lilivyostawi katika mazingira ya Dodoma. Wamesema ni mara yao ya kwanza kuona viazi mviringo vikilimwa na kustawi katika eneo hilo, huku wakionesha shauku ya kuanza kulima zao hilo pindi litakapothibitishwa rasmi.

Utafiti wa zao hilo mkoani Dodoma bado unaendelea ili kukamilisha hatua zote muhimu za kisayansi kabla ya mbegu hiyo kuingizwa rasmi sokoni.

Mafanikio ya jaribio hilo yanaendelea kuthibitisha uwezo wa Dodoma kuzalisha mazao mbalimbali ya chakula na biashara kupitia utafiti, ubunifu na matumizi ya teknolojia za kisasa za kilimo, hatua inayoweza kuongeza uzalishaji, kipato na fursa za kiuchumi kwa wakulima wa Mkoa wa Dodoma.

No comments:

Post a Comment