MICHEZO - OKULY BLOG

Breaking

Music

Header ADS

Friday, November 6, 2015

MICHEZO



TANNZANIA YAKWEA "JINO MOJA" VIWANGO FIFA. TANZANIA imekwea kwa nafasi moja katika viwango vipya vitolewavyo kila mwezi na Shirikisho la Soka Duniani-FIFA huku Uganda wakiendelea kuongoza kwa nchi za Afrika Mashariki na Kati.

Kwa orodha hiyo iliyotolewa leo Tanzania ndio wanaoburuza mkia kwa nchi za ukanda wa Afrika Mashariki wakishika nafasi ya 53 kwa upande wa Afrika huku majirani zutu Uganda wakiwa nafasi ya 14 na duniani wa 68, Rwanda nafasi ya 23 duniani wa 96, Kenya nafasi ya 48 duniani 125 na Burundi nafasi ya 40 duniani 107.

 Katika tano bora kwa upande wa Afrika, Ivory Coast ndio wanaoongoza kwasasa wakishikilia nafasi ya 22 wakifuatiwa na Algeria walioko nafasi ya 26, Ghana ni watatu wakiwa nafasi ya 30. CapeVerde wamekwea tena na kuingia tano bora za Afrika kwa kushikilia nafasi ya 32 duniani wakifuatiwa na Senegal walioko nafasi ya 39.

 Kwa ujumla duniani orodha hiyo sasa inaongozwa na Ubelgiji walioikwaa nafasi hiyo kutoka kwa Argentina ambao wameporomoka mpaka nafasi ya tatu, mabingwa wa dunia Ujerumani wao wako nafasi ya pili, Ureno nafasi ya nne na tano bora inakamilishwa na mabingwa Copa Amerika Chile.

MARCELO AWAPA MCHECHETO DUNGA NA BENITEZ.

 KOCHA wa timu ya taifa ya Brazil, Dunga na meneja wa Real Madrid Rafael Benitez wameingia katika mchecheto juu ya afya ya Marcelo baada ya kupata majeruhi ya msuli wa paja katika ushindi wa bao 1-0 iliyopata timu yake katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa Ulaya dhidi ya Paris Saint-Germain juzi.

 Beki huyo mwenye umri wa miaka 27 alitolewa katikati ya kipindi cha kwanza katika mchezo huo uliofanyika katika Uwanja wa Santiago Bernabeu. Sasa nyota huyo kuna hati hati ya kuukosa mchezo muhimu wa clasico dhidi ya mahasimu wao Barcelona na ule wa timu yake ya taifa ya Brazil wa kufuzu Kombe la Dunia dhidi ya Argentina utakaofanyika huko Buenos Aires.

Akihojiwa Benitez amesema Marcelo amekuwa akicheza mechi nyingi na walifahamu lolote linaweza kutokea ingawa walidhani anaweza kupata muda wa kutosha kufikia mapumziko ya kupisha mechi za kimataifa.

Benitez aliendelea kudai kuwa beki huyo aligundua tatizo lake mapema na kumtaarifu kabla ya kuamua kutoendelea na mchezo, na kwasasa wanasubiria vipimo kuona ukubwa wa tatizo. Brazil itakwaana na Argentina Novemba 12 kabla ya kuikaribisha Peru Novemba 17 huku ule mchezo wa clasico ukitarajiwa kuchezwa Novemba 21.

VIDEO YA NGONO YAMTESA BENZEMA.

MSHAMBULIAJI nyota wa kimataifa wa Ufaransa na klabu ya Real Madrid, Karim Benzema amewekwa rasmi chini ya uchunguzi leo akihusishwa na tuhuma za kulaghai ili kupata pesa kutoka kwa Mfaransa mwenzake Mathieu Valbuena wakitumia mkanda wa video wa ngono.
Taarifa ya waendesha mashitaka wa Versailles imedai kuwa tuhuma hizo za kihalifu ambazo zinachunguzwa inaweza kubeba adhabu ya miaka siyopungua mitano jela. Wakili wa Benzema, Sylvain Cormier aliwaambia wanahabari baada ya kusikilizwa kwa shitaka hilo kuwa mteja wake alikuwa hana hatia na hakuhusika kwa vyovyote vile na tukio hilo la kihalifu. Kesi hiyo imeanza kuleta wasiwasi juu ya ushiriki wa mchezaji huyo katika michuano ya Euro 2016 ambayo itafanyika nchini Ufaransa.


RAIS WA DORTMUND ATUPA TAULO KWA KUINYOOSHEA MIKONO BAYERN.

OFISA mkuu wa Borussia Dortmund, Hans-Joachim Watzke amedai klabu yao haiwezi kushindania taji la Bundesliga na Bayern Munich. Dortmund imekuwa katika kiwango kizuri toka ujio wa meneja mpya Thomas Tuchel wakishika nafasi ya pili katika msimamo wa ligi huku wakipoteza mchezo mmoja pekee katika mashindano yote msimu huu, ingawa mchezo huo ukiwa ule waliotandikwa mabao 5-1 na Bayern.

 Bayern kwasasa ndio wanaongoza ligi wakitofautiana na Dortmund kwa alama tano na Watzke anaamini mbio za ubingwa zimeshakwisha. Akihojiwa Watzke amesema haina maana yeyote kuzungumzia kuhusu kuifukuzia Bayern kwani mpaka sasa wameshapoteza alama pekee na kama wakiendelea hivyo wanaweza kuendelea kutanua pengo la alama hadi kufikia nane kwa msimu wote.

Watzke aliendelea kudai kuwa wanachoangalia wao kwasasa ni jinsi wanavyofanya kwani wameimarika sana toka ujio wa kocha mpya. Dortmund watakuwa wenyeji wa Qabala katika mchezo wa Europa League baadae leo kabla ya kurejea Jumapili hii katika Bundesliga kwa kukwaana na mahasimu wao wa Ruhr Schalke.

ENRIQUE AKIRI PAMOJA NA KUMKUMBUKA MESSI LAKINI KIKOSI CHAKE HAKIMTEGEMEI.

MENEJA wa Barcelona, Luis Enrique amekiri kikosi chake kinamkumbuka Lionel Messi lakini anaamini kwa matokeo ambayo wamekuwa wakipata kunaonyesha kabisa hawamtegemei mshambuliaji huyo wa kimataifa wa Argentina.

Barcelona iliibuka na ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya BATE katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa Ulaya uliochezwa jana kwa mabao yaliyofungwa na Neymar na Luis Suarez aliyefunga mawili.

Klabu hiyo ya Catalan ndio wanaongoza kundi E wakiwa na alama 10 katika michezo minne waliyocheza hivyo kuwafanya kuihitaji alama moja pekee katika mchezo wao dhidi ya AS Roma Novemba 24 ili waweze kufuzu hatua ya timu 16 bora.

 Messi aliumia goti Septemba 26 katika mchezo wa La Liga dhidi ya Las Palmas lakini ukosekana kwake kumeonekana kutokuwa na athari kubwa kwani mabingwa hao wa Hispania na Ulaya wamepoteza mechi moja katia ya nane walizocheza.
 Akihojiwa Enrique amesema ni kweli wanamkumbuka Messi lakini timu hiyo hiyo siku zote imekuwa na rasilimali ndio maana unaona wanaendelea kufanya vyema pamoja na kumkosa nyota wao.

WENGER AKIRI ARSENAL KUWA NA NAFASI FINYU YA KUSONGA MBELE LIGI YA MABINGWA ULAYA.

MENEJA wa Arsenal, Arsene Wenger amesema kikosi chake kina nafasi finyu ya kutinga hatua ya timu 16 bora katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya baada ya kugaragazwa kwa mabao 5-1 na Bayern Munich juzi.

 Kipigo hicho kinaiacha Arsenal mkiani mwa kundi F wakiwa alama sita nyuma ya vinara Bayern Munich na Olympiakos wanaoshika nafasi ya pili.

Arsenal sasa lazima wawafunge Dinamo Zagreb na Olymipakos katika mechi zao mbili za mwisho huku wakiomba Bayern waifunge Wagiriki hao katika mchezo wao. Akihojiwa mara baada ya mchezo huo Wenger amesema bado wana nafasi lakini wanatakiwa kutambua kuwa nafasi yenyewe ni finyu.

Kocha huyo aliendelea kudai kuwa pamoja na hayo bado wataendelea kupambana mpaka mwisho.


YAMTIMUA RAMSEY.

KLABU ya Queens Park Rangers-QPR imemtimua meneja wake Chris Ramsey ikiwa imepita miezi michache toka achukue mikoba ya kuinoa timu hiyo.

Ramsey mwenye umri wa miaka 53 ambaye alisaini mkataba wa miaka mitatu Mei mwaka huu baada ya kuitumikia timu hiyo kama kocha wa muda, alitimuliwa baada ya kipigo cha bao 1-0 dhidi ya Derby Count juzi ambacho kimewaacha wakining’inia katika nafasi ya 13 katika msimamo wa ligi.

Mkurugenzi wa michezo wa QPR Les Ferdinand alithibitisha taarifa hizo akidai kuwa kile walichokuwa wakikitegemea kutoka kwa kocha huyo hakukipata ndio maana wakaamua kuzitisha mkataba naye.

QPR waliteremka daraja kutoka Ligi Kuu Mei baada ya Harry Redknapp kujiuzulu kama meneja Februari na Ramsey kuchukua mikoba yake.

No comments:

Post a Comment