ALIYEKUWA Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, George Simbachawene, amekabidhi ofisi kwa Waziri Hamad Masauni, katika ofisi ya Wizara hiyo, Mtumba, Jijini Dodoma, leo Januari 17, 2022.
Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo, Simbachawene amemtakia majukumu mema Mhandisi Masauni katika utumishi wake na kuongeza kuwa, Waziri huyo anaijua vema Wizara hiyo hivyo Wizara ipo katika mikono salama.
“Nawashukuru sana Watendaji wote wa Wizara kwa ushirikiano mlionipa wakati wote niliokuwa nanyi katika uongozi wangu ndani ya Wizara hii, Waziri Masauni ana uzoefu mkubwa na Wizara hii na anaijua vema, namtakia majukumu mema katika uongozi wake,” alisema Simbachawene.
Kwa upande wake Waziri Masauni, alimshukuru Simbachawene ambaye sasa ni Waziri wa Katiba na Sheria, kwa kumkabidhi ofisi na pia amemuahidi kuendelea kufanya naye kazi kwa ukaribu.
Pia Waziri Masauni amewataka viongozi wa Wizara hiyo kufanya kazi kwa ubunifu na yupo tayari kusikiliza ushauri na milango ya ofisi yake ipo wazi.
“Tufanye kazi kwa ushirikiano na ubunifu, tumsaidie mheshimiwa Rais kujenga Taifa, nipo tayari kusikiliza ushauri kutoka kwenu,” alisema Masauni.
Baada ya makabidhiano hayo ya ofisi, Waziri Masauni alifanya kikao na Wakuu wa Taasisi na Wakuu wa Idara wa Makao Makuu ya Wizara yake, ambapo alisikiliza kero zao na kuahidi kuzifanyia kazi.
*Mwisho/-*
No comments:
Post a Comment