Na Okuly Julius - Dodoma
Kundi kubwa la vijana wa kuanzia miaka 15_24 linachangia maambukizi mapya ya Virusi vya UKimwi(VVU) ambapo vijana ndo wanaingia kwenye mambukizi mapya kwa wingi ambapo wanachukua asilimia 40%.
Hayo yamesemwa Leo Novemba 14,2023 jijini Dodoma na Waziri wa Nchi,Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera,Bunge na Uratibu),Mhe.Jenista Mhagama, wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu maandalizi ya maadhimisho ya siku ya UKIMWI Duniani 2023 yanayotarajia kufanyika katika uwanja wa jamuhuri mkoani Morogoro tarehe 1 Desemba.
Aidha amesema kuwa katika takwimu iliyofanyika inaonyesha kuwa kina Mama wamehamasika na kuvutiwa zaidi na kupima UKIMWI kuliko kina Baba,hivyo amewaasa kina baba kujitokeza kupima ili kuleta manufaa chanya kwenye familia na jamii kwa ujumla.
"Kina Baba wengi hawapendi kupima na wamekuwa wakiwaambia kina Mama wakawapimie wakidhani kwamba mama akipima na yeye anakuwa yuko sawa jambo ambalo sio sahihi kwani mama anaweza akawa hana maambukizi lakini baba akawa nayo hivyo ningewasihi kina baba wawe mstari wa mbele kujitokeza kupima UKIMWI na kujua afya zao ili kuweza kuanza dawa kwa wakati" Amesisitiza Mhe.Mhagama
Aidha ameongeza kuwa maadhimisho haya ya UKIMWI Duniani yataambatana na matukio mbalimbali ikiwemo mdahalo wa viongozi wa dini pamoja na mdahalo wa viongozi wa kijamii ambapo viongozi hao watapata fursa ya kukutanishwa na vijana kwenye mdahalo wa wazi ili kuweza kuongea na vijana.
"Kutakuw pia na kongamano la vyuo vikuu na vyuo vya kati na kufanyika hivyo na mikoa mingine ili kuwakutanisha vijana,tunaelewa pia vijana wanapenda michezo kupitia sekta hiyo kutakuwa na mbio ambazo zitafanyika tarehe 26 Morogoro ikiwa ni pamoja na kongamano la kisayansi tarehe 27- 28 "Ameongeza Mhe.Mhagama.
Aidha amewasihi watanzania haswa wazazi kukaa na wanafamilia kwa pamoja na kuja na mbinu mbadala na kuangalia namna gani ya kujikinga na kuthibiti UKIMWI na kutokomeza kabisa maambukizi mapya.
Kwa upande wake Dk.Anath Ruebembera Meneja Mpango wa taifa wa kuthibiti UKIMWI,Wizara ya Afya amesema upatikanaji wa vipimo vya kupima VVU vinapatikana kila mahali ikiwa ni pamoja na hospitali za serikali na sekta binafsi ambapo kwa sasa wameongeza kipimo kingine cha kujipima mwenyewe baadae kwenda kuhakikisha kwenye vituo vya afya.
" Upatikanaji wa Kondom tatizo ni kwamba zikizambazwa huwa zinachukuliwa kwa muda ule ule na hivi sasa tutaweka utaratibu wa mtu wa kutokutumia kondom zaidi ya moja mwisho iwe kondom 3 ili kila mtanzania imfikie maana wengine wamekuwa wakichukua na kwenda kuuza"Amesisitiza Dk.Anath
Naye Makamu Mwenyekiti wa watu wanaoishi na Virusi Vya Ukimwi VVU (NACOFA) Emanuel Reuben Msinga amesema kama taasisi wamekuwa wakifanya kazi kubwa ya kuwakusanya vijana kuanzia miaka 15 na kuendelea kuwapa Elimu juu ya umuhimu wa upimaji wa VVU na matumizi ya dawa za kufubaza virusi hivyo.
Mgeni Rasmi wa siku ya UKIMWI Duniani anatarajiwa kuwa Waziri Mkuu Mhe.Kassim Majaliwa ambapo kauli mbiu ya mwaka huu inasema"JAMII IONGOZE KUTOKOMEZA UKIMWI".
No comments:
Post a Comment