
Na Mwandishi Wetu, Dodoma
WAZIRI wa Madini, ,na mgombea ubunge Jimbo la Mtumba Anthony Mavunde amesema hakuna sababu ya vijana wa kiume kubezwa au kutazamwa kwa jicho la ajabu wanapoamua kujihusisha na kazi ya ususi, kwani ni kazi halali kama nyingine yoyote.
Amesema hayo jijini Dodoma katika uzinduzi wa Siku ya Wasusi, uliowakutanisha wasusi kutoka mikoa mbalimbali ya Tanzania Bara, ambapo alisisitiza kuwa jamii haina budi kuachana na mitazamo ya kudhalilisha kazi zinazofanywa na watu kwa bidii na maarifa yao.
Mavunde amesema kuwa kazi ya ususi imekuwa mkombozi kwa vijana wengi, hususan wanawake, lakini sasa pia imekuwa ikiwavutia baadhi ya vijana wa kiume, jambo linalopaswa kuungwa mkono badala ya kubezwa.
Ameongeza kuwa moja ya malengo yake ni kuhakikisha ususi unaboreshwa ili kuifanya kuwa kazi ya heshima na inayotambulika rasmi, huku serikali ikijiandaa kutoa mafunzo rasmi kwa vijana kupitia vyuo vya ufundi kama VETA.
"Tayari serikali imeanza kushirikiana na VETA kutoa kozi fupi za ususi kwa lengo la kuwawezesha vijana waliokuwa wakijifunza kienyeji kupata ujuzi rasmi, na hatimaye kujiajiri au kuajiriwa kwa ufanisi zaidi," Amesema .
Amesisitiza kuwa kazi yoyote halali inayomletea mtu kipato ni ajira, na hivyo jamii inapaswa kuwaheshimu watu wote wanaojishughulisha katika sekta hiyo badala ya kuwavunja moyo.

Katika hafla hiyo, Mkurugenzi wa Chido Point, Maria Mwampanga, ambaye ndiye aliyeratibu siku hiyo, amesema maadhimisho hayo yamelenga kuwajengea wasusi uwezo wa kujitambua, kuwaunganisha kwa pamoja kitaifa, na kuwasaidia kufikia serikali ili waweze kupata mikopo na fursa nyingine za kiuchumi.
Baadhi ya wasusi walioshiriki walieleza changamoto mbalimbali wanazopitia, zikiwemo dharau kutoka kwa jamii, kutengwa na baadhi ya taasisi za dini, pamoja na mazingira magumu ya kufanyia kazi.
Frank Mwingira, msusi kijana kutoka Jiji la Dar-es-Salaam amesema alianza kazi hiyo tangu akiwa mdogo kupitia familia ya wasusi, lakini alikumbana na vizingiti vingi kutoka kwa watu waliokuwa wakimkejeli kwa kuwa kijana wa kiume anayefanya kazi inayohusiana na wanawake.
Ameeleza kuwa licha ya changamoto hizo, aliendelea kufuatilia kipaji chake hadi sasa ambapo kazi hiyo imekuwa chanzo kikuu cha kumsaidia yeye na familia yake.
Naye Faustin Kwolesya kutoka mkoa wa Kilimanjaro alisema alianza kazi ya ususi miaka ya nyuma lakini alikumbana na upinzani kutoka kwa baadhi ya viongozi wa dini waliokuwa wakimshangaa kwa kukaa na wanawake muda mwingi. Hata hivyo, alisema hakurudi nyuma na sasa anaendelea kupata mafanikio makubwa kupitia kazi hiyo.
Hata hivyo maadhimisho hayo yamebeba ujumbe wa kuhamasisha jamii kuondoa unyanyapaa dhidi ya kazi za mikono, hususan zile zinazohusishwa kimakosa na jinsia fulani, huku serikali ikihimizwa kuwekeza zaidi katika kutoa mafunzo rasmi ya stadi za maisha kwa vijana.







No comments:
Post a Comment