WIZARA YA MALIASILI NA UTALII YAJIIMARISHA KISHERIA USIMAMIZI WA BIASHARA ZA UTALII NCHINI - OKULY BLOG

Breaking

Music

Header ADS

Wednesday, October 15, 2025

WIZARA YA MALIASILI NA UTALII YAJIIMARISHA KISHERIA USIMAMIZI WA BIASHARA ZA UTALII NCHINI



Na Sixmund Begashe, Dodoma


Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia Idara ya Utalii imeendelea kujiimarisha kisheria kwa kuwajengea uwezo Maafisa wake kupitia mafunzo maalum kuhusu Sheria na Kanuni za Usimamizi wa Biashara za Utalii nchini.

Akizungumza wakati wa mafunzo hayo jijini Dodoma, Mkurugenzi Msaidizi wa Sehemu ya Huduma za Utalii na Udhibiti Ubora, Richie Wandwi, amesema lengo ni kuongeza uelewa wa maafisa hao kuhusu tafsiri na utekelezaji wa sheria na kanuni zinazohusu sekta hiyo, sambamba na kuboresha huduma kwa wadau ili kupanua wigo wa fursa za biashara za utalii nchini.

Wandwi amewataka maafisa hao kutumia maarifa waliyopata kuimarisha utendaji kazi unaozingatia sheria, kanuni na taratibu kwa manufaa ya Taifa na ustawi wa sekta ya utalii kwa ujumla.

“Moja ya majukumu yetu kama Idara ni kusimamia biashara za utalii nchini. Tunatekeleza jukumu hili kwa mujibu wa sheria, kanuni na miongozo mbalimbali, hivyo tumeona ni muhimu kupata mafunzo haya ili kuongeza uelewa wa kisheria kwa maafisa wetu na kufanya kazi kwa ufanisi zaidi,” amesema Wandwi.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Kitengo cha Huduma za Sheria wa Wizara hiyo, Frederick Komba, ameipongeza Idara ya Utalii kwa kuandaa mafunzo hayo, akisema yatachochea uwajibikaji na ufanisi zaidi katika utekelezaji wa majukumu ya kila siku.

Mafunzo hayo, yaliyotolewa na wataalam kutoka Kitengo cha Huduma za Sheria cha Wizara hiyo, yamehusisha Maafisa Utalii kutoka Makao Makuu na ofisi za kanda mbalimbali nchini.


No comments:

Post a Comment