Wananchi wa Jimbo la Fuoni na Siha pamoja na Kata tano za Tanzania bara wamejitokeza kwa wingi kupiga kura leo Desemba 30,2025 katika Uchaguzi mdogo uliofanyika katika majimbo yao.
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji wa Rufaa Mhe. Jacobs Mwambegele leo Desemba 30,2025 ametembelea na kushuhudia zoezi la upigaji kura katika Jimbo la Fuoni lililopo Wilaya ya Magharibi B, Mkoa wa Mjini Magharibi, Tanzania Zanzibar na kusema zoezi hilo linakwenda vizuri na wananchi wamejitokeza kwa wingi licha ya asubuhi kuwa na mvua.
Aidha, Jaji Mwambegele amesema katika Jimbo la jimbo la Siha lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Siha, Mkoa wa Kilimanjaro, Tanzania Bara ambako nako uchaguzi wa Mbunge unafanyika zoezi hilo linakwenda vizuri.
Jaji Mwambegele amesema, uchaguzi mdogo huo unahusisha pia, kata tano za Tanzania Bara ambazo ni Chamwino iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro, Mkoa wa Morogoro; Mbagala Kuu iliyopo Halmashauri ya Manispaa ya Temeke, Mkoa wa Dar es Salaam; na Nyakasungwa iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Buchosa, Mkoa wa Mwanza.
Kata nyingine ni Kata ya Masoko iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, Mkoa wa Mbeya; na kata ya Ndono iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Uyui, Mkoa wa Tabora.
Mwenyekiti huyo wa Tume katika ziara hiyo aliambatana na Mjumbe wa Tume Mhe. Magdalena Rwebangira.

No comments:
Post a Comment