
Wakati anamsifia mpenzi wake Msanii Mbosso aliimba “ _Kamusi namaliza kurasa kukusifia”_ ,na akahitimisha kwa kusema anaishiwa pawa kwa kuwa penzi la huyo ampendaye ni mizani nzito.
Mbosso angepata fursa ya kupanda mlima Lolmalasin uliopo Ngorongoro kamwe asingeishiwa pawa, badala yake angeongeza maneno katika kamusi kuusifia mlima huu unaopatikana katika kivutio namba moja cha utalii barani Afrika.
Angeusifia mlima huu kwa kuwa ni mlima mrefu zaidi ndani ya Hifadhi ya Ngorongoro na mlima wa tatu kwa urefu Tanzania, ukiwa na kimo cha mita 3,700 kutoka juu ya usawa wa bahari.
Angepanda mlima huu asingeweza kuishiwa pawa kutokana na mandhari yaliyopambwa na maua, miti, ndege, wanyama huku akishuhudia Kreta ya Olmoti kwa mbali ikitiririsha maji yake kwenda Kreta ya Ngorongoro kupitia mto Munge.
Mlima huu si mzuri tu kupanda laah hasha, unakusaidia kupiga jaramba na kunyoosha misuli hasa kwa wanaojiandaa kukwea Milima mirefu kama Meru na Kilimanjaro.
Ukipanda mlima huu si tu unajenga afya na kupanua mawanda ya upeo wa macho na akili yako, bali utahisi upo peponi na kusahau changamoto zote ikiwemo Stress za ada za januari, vikoba, kazi na hata mapenzi.
Na kama Mbosso alisema kwamba yeye ni Mjusi anaparamia ukuta wa plasta basi hata watalii kutoka maeneo mbalimbali wanaweza kuupanda mlima huu bila kuuparamia na wala hawataishiwa Pawa kamwe.
Karibuni wageni kupanda mlima Lolmalsin, Ngorongoro inawahakikishia kutoishiwa pawa na badala yake pawa zitaongezeka maradufu.
Tuishie hapa kwa methali isemayo " _Kinywa ni Jumba la Maneno_ " kesho kutoka Ngorongoro tutakuletea maneno ya kivutio kingine cha utalii kwa kuwa "Jungu kuu halikosi ukoko"
Maajabu ya Ngorongoro yanakuita,
Uzoefu usiosahaulika,
Tumerithishwa, Tuwarithishe



No comments:
Post a Comment