TRUMP AIPA IRAN NAFASI YA MWISHO - OKULY BLOG

Breaking

Music

Header ADS

Tuesday, March 24, 2026

TRUMP AIPA IRAN NAFASI YA MWISHO


Rais wa Marekani, Donald Trump, amesema kuwa Iran ina “nafasi moja zaidi” ya kufikia amani, huku kukiwa na mkanganyiko kuhusu uwepo wa mazungumzo kati ya pande hizo mbili.

Kupitia ujumbe wake kwenye mitandao ya kijamii, Trump alidai kuwa Marekani na Iran zimekuwa na mazungumzo kuhusu “suluhisho kamili la kumaliza uhasama” katika eneo la Mashariki ya Kati. Aidha, alisema ameahirisha mashambulizi aliyokuwa ametishia kuyafanya dhidi ya miundombinu ya nishati ya Iran kwa muda wa siku tano.

Hatua hiyo ilichangia kushuka mara moja kwa bei za mafuta na gesi katika masoko ya dunia.

Hata hivyo, Iran imekanusha vikali madai hayo. Spika wa Bunge la nchi hiyo, Mohammad-Bagher Ghalibaf, amesema hakuna mazungumzo yaliyofanyika na kudai kuwa taarifa hizo ni “habari za uongo” zinazolenga kuathiri na kudanganya soko la mafuta.

Pamoja na msimamo huo wa Iran, afisa mwandamizi wa wizara ya mambo ya nje ya nchi hiyo amenukuliwa akisema kuwa wamepokea mapendekezo kutoka Marekani kupitia wapatanishi, na kwamba yanapitiwa. Hata hivyo, alisisitiza kuwa hatua hiyo ni maandalizi ya awali na si uthibitisho wa mazungumzo rasmi yanayoendelea.

Ripoti mbalimbali zimeendelea kutofautiana kuhusu suala hilo. Baadhi ya vyanzo kutoka Marekani vinadai kuwa mazungumzo yalifanyika kwa njia isiyo ya moja kwa moja yakiwahusisha wajumbe wa karibu wa Trump, huku taarifa nyingine zikieleza kuwa nchi kama Misri, Uturuki na Pakistan zilihusika kama wapatanishi.

Wakati huo huo, Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu, ameunga mkono uwezekano wa kufikiwa kwa makubaliano, akisema hatua hiyo inaweza kusaidia kufanikisha malengo ya operesheni ya pamoja kati ya Marekani na Israel.

Hali hii inajiri wakati mvutano katika eneo hilo ukiendelea kuongezeka, hasa baada ya mashambulizi kulenga pia miundombinu ya kiuchumi kama vituo vya gesi. Wataalamu wanasema hatua hiyo imeongeza hofu kuhusu usalama wa nishati na uthabiti wa uchumi wa kimataifa.

No comments:

Post a Comment