Serikali imeeleza kuwa itaendelea kuwekeza katika sekta ya elimu ya juu ili kuzalisha wataalamu wenye ujuzi, kuongeza ushindani wa uchumi na kuchochea maendeleo endelevu ya Taifa.
Hayo yameelezwa na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), wakati wa hafla ya uwekaji wa jiwe la msingi la ujenzi wa Jengo la Taaluma la Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA), Kampasi ya Singida, chini ya Mradi wa Mageuzi ya Kiuchumi kwa Vyuo vya Elimu ya Juu (HEET), ambapo Mgeni Rasmi alikuwa Waziri Mkuu, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba
Mhe. Munde alisema kuwa, Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeifanya elimu kuwa sekta ya kimkakati katika kujenga uchumi wa kisasa unaoweza kushindana kimataifa.
“Uwekezaji unaoendelea katika vyuo vya elimu ya juu, Serikali inalenga kuongeza upatikanaji wa elimu bora, kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia, kuimarisha tafiti, ubunifu na matumizi ya teknolojia pamoja na kuzalisha wataalamu watakaotekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo”, alisema Mhe. Munde.
Alieleza kuwa, Mradi wa HEET ni mfano wa uwekezaji unaolenga kuimarisha rasilimali watu, kuongeza tija katika uzalishaji na kuimarisha ushindani wa uchumi wa Tanzania kwa muda mrefu.
"Kila shilingi inayowekezwa katika elimu ni uwekezaji unaorudisha faida kupitia ongezeko la ujuzi, ajira, uzalishaji na mapato ya Taifa," alisisitiza Mhe. Munde.
Aidha, alisema kukamilika kwa jengo hilo kutaiwezesha Kampasi ya TIA Singida kuongeza uwezo wa kudahili wanafunzi wengi zaidi, kuboresha mazingira ya kujifunzia na kuimarisha utoaji wa mafunzo katika fani za uhasibu, fedha na biashara.
Aliongeza kusema kuwa, mradi huo pia utachochea shughuli za kiuchumi katika Mkoa wa Singida kupitia ajira, biashara na huduma mbalimbali zitakazozunguka Kampasi hiyo.
Kadhalika, alisema kuwa, Wizara ya Fedha itaendelea kuhakikisha rasilimali za fedha zinazopatikana kupitia ushirikiano na washirika wa maendeleo zinaelekezwa katika miradi inayochochea ukuaji wa uchumi ili kuleta tija kwa wananchi.
Kuhusu usimamizi wa fedha za umma, Naibu Waziri alisisitiza kuwa Serikali inatarajia mradi huo kukamilika kwa wakati, kuzingatia viwango vya ubora, kutekelezwa ndani ya gharama zilizoidhinishwa na kutoa thamani halisi ya fedha.
Alimtaka Mkandarasi, Mshauri elekezi na wasimamizi wa mradi kuzingatia masharti ya mkataba, kuhakikisha ubora wa kazi, kutumia nguvu kazi ya ndani pale inapowezekana pamoja na kulinda usalama wa wafanyakazi na mazingira.
Vilevile, aliutaka uongozi wa TIA kusimamia ipasavyo miundombinu hiyo baada ya kukamilika ili idumu kwa muda mrefu na kuendelea kutoa huduma bora za elimu, sambamba na kuandaa wahitimu wenye maadili, ubunifu na ujuzi unaokidhi mahitaji ya uchumi wa Taifa.
Naibu Waziri Mhe. Munde, aliipongeza Serikali, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, uongozi wa TIA, washirika wa maendeleo, mkandarasi na wadau wote waliofanikisha hatua hiyo muhimu, huku akiahidi kuwa Wizara ya Fedha itaendelea kushirikiana na taasisi mbalimbali kuhakikisha miradi ya kimkakati inayochochea maendeleo ya uchumi na ustawi wa wananchi inatekelezwa kwa ufanisi.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Ushauri ya Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA) Prof. Jehovaness Aikael na Afisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya TIA, Prof. William Pallangyo, waliishukuru Serikali kwa jitihada zake za kufanikisha ujenzi wa jengo hilo ambalo limekamilika kwa asilimia 63.
Alisema kuwa kukamika kwa jengo hilo kutaifanya Kampasi hiyo kuongeza Wanafunzi kutoka 2600 hadi zaidi ya 5000, jambo litakalotoa fursa zaidi kwa vijana kutoka Mkoa huo na maeneo mengine ya nchi kupata elimu.
Walisema Kampasi ya Singida ni ya muda mrefu katika kuanzishwa kwake toka mwaka 1974 ikitanguliwa na Kampasi ya Dar es Salaam, hivyo ni muda mwafaka wa Kampasi hiyo kujiimarisha kwa miundombinu ili kuweka mazingira bora zaidi ya wanafunzi kupata elimu.
Aidha waliiomba Serikali kuendelea kuongeza miundombinu ya mabweni ili kukidhi idadi kubwa ya Wanafunzi waliopo na wanaotarajiwa kuongezeka baada ya Jengo hilo kukamilika kwa kuwa kwa sasa wengi wanaishi nje ya Chuo hicho.










No comments:
Post a Comment