TANZANIA YAUNGA MKONO MKATABA MPYA WA KIMATAIFA WA KULINDA WAFANYAKAZI WA MTANDAONI - OKULY BLOG

Breaking

Music

Header ADS

Friday, June 12, 2026

TANZANIA YAUNGA MKONO MKATABA MPYA WA KIMATAIFA WA KULINDA WAFANYAKAZI WA MTANDAONI

Na: OWM (KAM) – Geneva, Uswisi

Ujumbe wa Tanzania umeunga mkono Mkataba mpya wa Kimataifa unaolenga kulinda haki, usalama na ustawi wa Wafanyakazi wa Mtandaoni ikiwa ni dhamira ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika kuhakikisha maendeleo ya teknolojia na majukwaa ya kidijitali yanakwenda sambamba na ulinzi wa utu wa mfanyakazi, usawa na haki za msingi za kazi.

Hayo yamejiri wakati wa hafla ya kuhitimisha Mkutano Mkuu wa 114 wa Shirika la Kazi Duniani (ILO) leo tarehe 12 Juni, 2026 iliyofanyika katika Ukumbi wa Umoja wa Mataifa, Jijini Geneva, Uswisi ambapo kupitia Mkutano huo, taarifa za Kamati mbalimbali zilipokelewa ikiwemo Kamati ya Upangaji wa Viwango vya Kazi ambayo imewezesha kuandaliwa na kupitishwa kwa Mkataba wa Kazi kuhusu Wafanyakazi Mtandaoni wa Mwaka 2026.

Katika kupitisha Mkataba huu, kura 406 zimeunga mkono kupitishwa kwa Mkataba husika, nchi Nane (8) hazijaunga mkono kupitishwa Mkataba na nchi 36 hazijaonesha kuwa upande wowote. Mkataba huo mpya umeweka misingi ya kimataifa kuhusu: Ulinzi wa haki za msingi za wafanyakazi wa mtandaoni; Uainishaji sahihi wa hadhi ya ajira kulingana na hali halisi ya kazi; Malipo ya haki na uwazi; Upatikanaji wa hifadhi ya jamii; Uwazi na udhibiti wa mifumo ya kidijitali ikiwemo haki ya maelezo na mapitio ya maamuzi yanayofanyika kidijitali pamja na Ulinzi wa taarifa binafsi na haki ya kupata kusuluhisha migogoro.

Akitoa Hotuba yake wakati wa kufunga Mkutano huo, Rais wa Mkutano Mkuu wa 114 wa ILO, Juan Castillo, amesisitiza kuhusu mafanikio makubwa yaliyopatikana kupitia makubaliano ya kihistoria kuhusu kazi za staha kwa kazi zinazofanyika kidijitali.

Amesema, kutokana na ukuaji wa sayansi na teknolojia, kumekuwa na ongezeko kubwa la matumizi ya Akili Unde (AI), hivyo, amesisitiza kwamba teknolojia inapaswa kutumika ili kuendeleza ustawi wa binadamu na si kuondoa utu wa wafanyakazi au kuongeza ukosefu wa usawa, huku akihimiza matumizi ya Akili Unde yanayozingatia maadili na haki za kazi.

Kwa upande mwengine, Juan Castillo amepongeza mfumo wa Utatu wa Shirika la Kazi Duniani (ILO) umekuwa ni chombo muhimu cha kuwaleta pamoja waadau husika, yaani Serikali, Waajiri na Wafanyakazi, akieleza kuwa majadiliano na mafikiano yaliyofikiwa katika siku 12 za Mkutano huo yamethibitisha umuhimu wa mazungumzo ya kijamii katika kukuza ustawi wa Sekta ya Kazi.

Upitishwaji wa Mkataba wa Kazi Kuhusu Wafanyakazi wa Mtandaoni haumaanishi kuanza kwa utekelezaji wa baadhi ya masuala yaliyoanishwa katika Mkataba huo kwa kuwa Serikali ya Awamu ya Sita kupita Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano pamoja na Wadau wengine wa masuala ya Kazi, ilishaanza kutekeleza viwango vilivyotajwa katika Mkataba huo ambapo miongoni mwa jitihada zilizochukuliwa ni pamoja na: Kukuza na kutambua wafanyakazi wa mitandaoni kwa kuimarisha uchumi wa kidijitali; Kuimarisha ulinzi wa matumizi ya mtandao kupitia Sheria na miongozo kama vile Sheria ya Makosa ya Mtandaoni na Kanuni za Ulinzi wa Taarifa Binafsi.

Aidha, utoaji wa mafunzo ya TEHAMA kwa vijana yanalenga kuongeza fursa za ajira za kidijitali na kuwasaidia wafanyakazi wa mitandaoni kufanya kazi kwa ufanisi zaidi na kuingia kwenye soko la kimataifa na uimarishaji wa mifumo ya kidijitali umeendelea kupanua miundombinu ya TEHAMA kama vile upanuzi wa mtandao wa Vijijini na Mijini ili kuwezesha watu wengi zaidi kufanya kazi mtandaoni kwa ufanisi.

Mkutano Mkuu wa 114 wa Shirika la Kazi Duniani (ILO) umihitimishwa leo na kukamilika kwake ni mwanzo wa Kikao cha 357 cha Bodi ya Magavana ya ILO unaofanyika tarehe 12 na 13 Juni, 2026 Geneva, Uswisi ambapo Tanzania pia ni Mjumbe wa Bodi hiyo ikiwakilisha nchi za Ukanda wa Afrika Mashariki.

No comments:

Post a Comment