
Na: OWM – KAM, Dar es Salaam
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu amesema Serikali itaendelea kuweka mazingira wezeshi ya kuongeza fursa za ajira ndani na nje ya nchi kwa Watanzania kupitia maboresho ya Sera, Sheria, Kanuni na Miongozo.
Aidha, alibainisha kuwa kupitia juhudi za kidiplomasia za Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan zimeendelea kuzaa matunda, ambapo ndani ya kipindi kifupi cha awamu yake ya pili, vijana 8,408 wameweza kuunganishwa na fursa za ajira nje ya nchi, idadi ambayo ni kubwa kuwahi kufikiwa nchini.
Mhe. Sangu amesema hayo wakati wa hafla ya kuwaaga vijana wanaokwenda kufanya kazi nje ya nchi, Waziri mwenye dhamana ya Ajira, Ridhiwani Sangu, alisema Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan anatambua kuwa ajira ni nguzo muhimu ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi, kwani huchangia kuongeza kipato cha wananchi, kupunguza umasikini, kuimarisha ustawi wa jamii na kukuza uchumi wa taifa.
Amesema, Serikali pia inatambua ajira za nje ya nchi kama mkakati muhimu wa kupanua fursa za ajira kwa vijana wa Kitanzania, huku zikiwapa nafasi ya kupata kipato, kujenga taaluma, kuongeza ujuzi na uzoefu wa kazi pamoja na kujifunza teknolojia na mbinu bora zinazotumika katika masoko ya kimataifa.
Vile vile, Waziri Sangu ametoa wito kwa vijana hao kutumia vyema kipato watakachopata kwa kujifunza elimu ya fedha na kushirikiana na taasisi za kifedha ili kujiwekea akiba kwa ajili ya maendeleo yao ya baadaye. Pia aliwahimiza kujiunga na Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) kupitia mpango wa Hifadhi Scheme ili kujijengea usalama wa maisha baada ya kumaliza ajira zao.
Kadhalika, amewahamasisha vijana hao kuwa mabalozi wazuri wa Tanzania katika nchi wanazokwenda kufanya kazi, hivyo wanapaswa kuzingatia maadili, uadilifu, bidii katika kazi, kuheshimu sheria, tamaduni na mila za nchi hizo, huku wakidumisha utamaduni na maadili mema ya Kitanzania.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Kitengo cha Huduma za Ajira, Jane Sorogo, amesema vijana hao wanaliopata nafasi za ajira katika nchi ya Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), Saudi Arabia, Qatar, Kuwait, Bosnia na Ujerumani wameweza kupatiwa mafunzo maalumu kabla ya kuondoka nchini ili kuwajengea uelewa kuhusu haki na wajibu wao, pamoja na kutambua mila na desturi za nchi wanazokwenda kufanya kazi.
Akizungumza kwa niaba ya vijana wenzake, Husna Seif aliyepata fursa ya kwenda kufanya kazi nchini Saudi Arabia kama Mhudumu wa Usafi katika hoteli, ameishukuru Serikali kwa watafutia fursa za ajira na amesema ajira hizo zitawawezesha kupata ujuzi, kukua kiuchumi na kuboresha hali ya maisha ya familia zao.
Naye kijana Ally Mwajei, ameshukuru Serikali kwa kumwezesha kupata fursa ya kwenda kufanya kazi nchini kama dereva teksi, amesema anafurahia kupata nafasi hiyo kwa kuwa itampa fursa ya kutimiza malengo yake ya maisha, kujifunza mazingira mapya pamoja na mila na tamaduni tofauti. Amesema anaamini uzoefu atakaoupata nje ya nchi utamjengea uwezo na kumuinua kimaendeleo. Aidha, amewashauri vijana wenzake wasiache kuomba nafasi za ajira kila zinapotangazwa, kwani zinaweza kuwa mwanzo wa mafanikio yao.







No comments:
Post a Comment