Wananchi mkoani Mtwara wameishukuru Serikali kwa kuendelea kujenga na kuboresha miundombinu ya huduma za afya, hatua iliyowarahisishia upatikanaji wa huduma hizo bila kulazimika kusafiri umbali mrefu.
Hayo yamejiri Agosti 12, 2026, katika siku ya tatu ya ziara ya kikazi ya Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga (Mb), mkoani humo, yenye lengo la kukagua na kuzindua miradi mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa na Serikali ya Awamu ya Sita.
Wananchi hao wamesema wanapata huduma za afya kwa wakati na kwa urahisi, jambo walilolieleza kuwa limepunguza changamoto ya kufuata matibabu katika maeneo ya mbali.
Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Waziri Kapinga amesema Serikali inalenga kuboresha huduma za afya ili wananchi wapate matibabu kwa urahisi na kuendelea na shughuli zao za uzalishaji, hivyo kuimarisha uchumi wa familia na Taifa.
Amesema kusogeza huduma za afya karibu na wananchi ni sehemu ya juhudi za Serikali kuhakikisha wananchi wanapata huduma muhimu kwa wakati.
Aidha, amewataka wananchi kuendelea kushirikiana na Serikali katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo, akisisitiza kuwa ushirikiano ni msingi wa maendeleo.
Katika siku ya tatu ya ziara hiyo, Waziri Kapinga ametembelea miradi mbalimbali katika Majimbo ya Nanyamba, Mtwara Mjini na Mtwara Vijijini, ikiwemo kuzindua Kituo cha Afya Msangamkuu, kuzindua mabweni mawili na kutoa taulo za kike kwa wanafunzi wa Shule ya Wasichana Mtwara, kukagua ujenzi wa Shule ya Amali Chikota, pamoja na kutembelea Wodi ya Wazazi katika Hospitali ya Wilaya ya Tandahimba.






















No comments:
Post a Comment