
📌Ni kupitia Tuzo za Uandishi wa Habari za Samia Kalamu Awards
📌Wizara ya Nishati yatambua mchango wake
📌 Yamzawadia fedha taslimu, jiko linalotumia umeme kidogo, kompyuta mpakato na uniti za umeme za mwaka mmoja
📌 Mhandisi Mramba asema Tuzo ni kielelezo cha kuunga mkono juhudi za Rais Samia uhamasishaji Nishati Safi ya Kupikia
Nyamguma Mahamud, Mwandishi wa Habari kutoka Mlimani FM ameibuka kidedea katika Tuzo za Uandishi wa Habari za Samia Kalamu Awards 2025 kupitia kipengele cha habari za Nishati Safi ya Kupikia ambapo Wizara ya Nishati imetambua mchango wake kwa kumpa zawadi mbalimbali ili kuendelea kuhamasisha utoaji wa elimu ya Nishati Safi ya Kupikia.
Hafla ya utoaji wa Tuzo hizo imefanyika jijini Dar es Salaam huku mgeni rasmi akiwa ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Mohamud amekabidhiwa zawadi zake na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mhandisi Felchesmi Mramba kwa niaba ya Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko.
Mshindi huyo amekabidhiwa fedha taslimu shilingi milioni tano, kompyuta mpakato, jiko linalotumia umeme kidogo na uniti za umeme za mwaka mzima.
"Tunatambua masuala aliyoyaandika katika kuhamasisha nishati safi ya kupikia, kwahiyo tumemzawadia pia jiko la umeme la kisasa linalotumia umeme mdogo pamoja na umeme wa kutumia nyumbani kwake kwa mwaka mmoja," amesema Mha. Mramba
Amesema Tuzo ya Nishati Safi ya Kupikia ni kielelezo cha kuunga mkono juhudi za Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia.
Samia Kalamu Awards imeandaliwa na Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA) na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) ikiwa na kaulimbiu ya "Uzalendo Ndio Ujanja'





No comments:
Post a Comment