Migogoro ya Familia na Mila Kandamizi Zatajwa Kuvuruga Malezi, Elimu na Ndoto za Watoto Vijijini - OKULY BLOG

Breaking

Music

Header ADS

Monday, June 2, 2025

Migogoro ya Familia na Mila Kandamizi Zatajwa Kuvuruga Malezi, Elimu na Ndoto za Watoto Vijijini


Na Dotto Kwilasa, Dodoma


Kukosekana kwa maelewano kati ya baba na mama ndani ya familia kunatajwa kuwa chanzo kikubwa cha watoto wengi vijijini kukosa haki zao za msingi, ikiwemo malezi bora na fursa ya kupata elimu, hali inayowasukuma kujiingiza kwenye makundi hatarishi na kuacha masomo.

Hayo yamebainika mwishoni mwa wiki katika mdahalo wa kijamii uliofanyika katika Kijiji cha Kidoka, wilayani Chemba, mkoani Dodoma, ambapo viongozi wa kimila, viongozi wa dini, akina mama, vijana, pamoja na wawakilishi wa serikali za vijiji na mashirika ya kiraia walijadili kwa kina changamoto zinazokwamisha usawa wa kijinsia na ustawi wa familia.

Mdahalo huo uliandaliwa kupitia mradi wa Tuinuke kwa Pamoja kwa ufadhili wa Ubalozi wa Ireland, ambapo washiriki walisema kuwa familia nyingi zimepoteza mwelekeo kutokana na migogoro ya wazazi, hali ambayo huathiri maendeleo ya watoto, hususan elimu na malezi bora.

“Tumeona watoto wengi wa kiume na wa kike wakijihusisha na biashara za pombe, kuuza miili yao, na wengine kukimbilia mijini kusaka ajira zisizo rasmi,wote hawa ni waathirika wa migogoro ya nyumbani,” amesema Mzee Ahumani Twalib, mmoja wa wazee wa kijiji.

Naye Hamida Ndwatta ameeleza kuwa uwepo wa vilabu vya pombe kwenye makazi ya watu kumechangia wazazi Wengi kuishia kuwa walevi na kushindwa kutimiza majukumu yao ya malezi.

Amesema kuwa baadhi ya mila na desturi kama unyago na jando zimegeuka kuwa chanzo cha mimba za utotoni, utoro wa shule, na ndoa za utotoni, mambo yanayovunja kabisa ndoto za vijana wengi wa vijijini.

" familia ni msingi wa maendeleo ya mtoto, hivyo ni muhimu kuhakikisha kuwa wazazi wanapata elimu ya malezi na kushirikiana kwa usawa ili kujenga kizazi chenye maadili na uwezo wa kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya taifa, "ameeleza

Kwa ujumla ameeleza kuwa ustawi wa familia si suala la huduma pekee, bali linahitaji jitihada za kijamii, kimila, kielimu na kiuchumi ili kumjenga mtoto wa Tanzania anayejitegemea na kuchangia katika maendeleo endelevu. 

No comments:

Post a Comment