
Na Augusta Njoji, Handeni TC
MKUU wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese, amewataka Maofisa Mifugo wa Halmashauri ya Mji Handeni kutumia vishikwambi walivyokabidhiwa na serikali kwa kazi za kiofisi pekee na si kwa matumizi binafsi.
Akizungumza Septemba 22, 2025 wakati wa ugawaji wa vifaa hivyo mjini Handeni, Nyamwese amesema vishikwambi hivyo vimetolewa ili kuongeza ufanisi katika utendaji kazi na kusaidia harakati za utambuzi wa mifugo.
“Tusije tukasikia vinaingia kwenye matumizi ya mitandao ya kijamii kama ku stream live, kuingia youtube, instagram, facebook. Vishikwambi hivi vitumike kutekeleza majukumu yaliyokusudiwa,” amesema.
Ameongeza kuwa vifaa hivyo vitunzwe na changamoto zozote ziwasilishwe Kitengo cha TEHAMA cha Halmashauri badala ya kupelekwa kwa mafundi wa mtaani.
Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, Gerald Kauki, amesema hatua hiyo itawaongezea maofisa ufanisi katika kutoa huduma kwa wafugaji.
Naye, Mkuu wa Divisheni ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi wa Halmashauri hiyo, Aldegunda Matunda, amesema Halmashauri ina maofisa mifugo 27 wanaohudumia wafugaji 34,484 wenye mifugo zaidi ya 148,000.
Amefafanua kuwa katika mpango wa chanjo ya mifugo, Halmashauri imepokea vishikwambi 25 kutoka serikalini ambapo awali walikuwa na vishikwambi viwili pekee katika utambuzi wa mifugo.
“Utambuzi wa ng’ombe umefikia asilimia 58 na mbuzi asilimia 17. Tunaamini vifaa hivi vitachochea kasi ya utekelezaji wa mpango huo,” amesema.








No comments:
Post a Comment