UMEME UNACHOCHEA UCHUMI, AJIRA NA LISHE KWA WANANCHI WA VIJIJINI – RC PWANI - OKULY BLOG

Breaking

Music

Header ADS

Wednesday, January 28, 2026

UMEME UNACHOCHEA UCHUMI, AJIRA NA LISHE KWA WANANCHI WA VIJIJINI – RC PWANI




Na Mwandishi Wetu - Kibaha, Pwani


Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mhe. Abubakar Kunenge leo, tarehe 28 Januari, 2026 wakati wa hafla ya kuwatambulisha wakandarasi wa kampuni ya Nakuroi Ltd; kampuni iliyoshinda zabuni ya mradi wa kusambaza umeme katika vitongoji 330 vya mkoa huo, mradi wenye thamani ya shilingi bilioni 46.6.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mkuu wa Mkoa amesema umeme ni nguzo muhimu katika kukuza uchumi wa Mtanzania mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla sawa sawa lengo la Dira ya Maendeleo ya Taifa ya mwaka 2025/2050; inayolenga kuzalisha ajira zaidi ya milioni 8.5.

Amesema kupatikana kwa umeme vitongojini, kutapunguza wimbi la vijana kuhamia mijini, kwa kuwa watapata fursa za kiuchumi kupitia shughuli za uzalishaji huko kuko vitongoji, kwa ajili ya kuongeza kipato chao.

“Upatikanaji wa umeme vitongojini, utasaidia Wananchi kujiajiri, kukuza biashara ndogo ndogo na kuboresha maisha yao kwa ujumla,” amesema Mhe. Kunenge.

Aidha, amesema umeme una mchango mkubwa katika kuboresha lishe bora, hususan kwa watoto, kwa kuwa familia zitaweza kuandaa chakula chenye viwango bora na vyenye virutubishi. Ameeleza kuwa siku 1,000 za mwanzo tangu mtoto kuzaliwa ni muhimu kwa ukuaji na maendeleo ya mtoto, hivyo umeme ni nyenzo muhimu katika kuhakikisha hilo linatimia.

Kwa upande wake, Mhandisi, Thomas Mmbaga, Kaimu Mkurugenzi wa Umeme Vijijini kutoka Wakala wa Nishati Vijijini; amesema kuwa REA imekabidhi rasmi mradi huo kwa mkandarasi mzawa ili kutekeleza jukumu la kufikisha umeme katika vitongoji 330 vya mkoa wa Pwani.

Amesema mradi huo utatekelezwa kwa kipindi cha miaka mitatu na utaunganisha Wateja wa awali 10,706 huku Kaya ambazo hazitakuwa na uwezo wa kutandaza umeme majumbani (Wiring) zitapewa kifaa cha Umeme Tayari (UMETA); ambapo jumla ya vifaa vya UMETA 990 vimetengwa kwa mkoa wa Pwani.

Mhandisi, Mmbaga ameongeza kuwa baada ya kukamilika kwa vitongoji 330 vitasalia vitongoji 365 pekee katika mkoa huo, ambavyo REA imepanga kuvifikishia umeme kabla ya mwaka 2030.

Naye mwakilishi wa kampuni ya Nakuroi Ltd, Mhandisi, Nestory Vincent, amesema kampuni hiyo itashirikiana kwa karibu na Serikali pamoja na Wadau wote, wakiwemo REA ili kuhakikisha mradi unakamilika kwa wakati na kwa viwango vinavyoainishwa kwenye mkataba.

“Tumejipanga kutekeleza mradi huu kwa ufanisi mkubwa ili kufikisha umeme katika vitongoji 330 ili tuchangie maendeleo ya Wananchi wa Mkoa wa Pwani.” Amekaririwa, Mhandisi, Vincent.




No comments:

Post a Comment