NDEJEMBI: UPATIKANAJI WA NISHATI SAFI TANZANIA UMEONGEZEKA MARA TATU NDANI YA MIAKA MINNE - OKULY BLOG

Breaking

Music

Header ADS

Wednesday, February 18, 2026

NDEJEMBI: UPATIKANAJI WA NISHATI SAFI TANZANIA UMEONGEZEKA MARA TATU NDANI YA MIAKA MINNE

Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, akizungumza Februari 18,2026 katika Mdahalo wa Ngazi ya Juu wa Mawaziri ulioandaliwa na
Shirika la Kimataifa la Nishati (IEA) jijini Paris, Ufaransa


Na Mwandishi Wetu - PARIS


UPATIKANAJI wa nishati safi ya kupikia nchini Tanzania umeongezeka
kutoka asilimia 6.9 mwaka 2021 hadi asilimia 23.2 mwaka 2025, sawa na
ongezeko la zaidi ya mara tatu ndani ya kipindi cha miaka minne.

Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, amesema mafanikio hayo
yanaakisi dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita katika kuhakikisha
wananchi wanapata nishati safi, salama na nafuu kwa ajili ya kupikia,
huku yakichangia kulinda afya za wananchi, mazingira na kukuza uchumi
wa taifa.

Akizungumza Februari 18, 2026 katika Mdahalo wa Ngazi ya Juu wa
Mawaziri ulioandaliwa na Shirika la Kimataifa la Nishati (IEA) jijini
Paris, Waziri Ndejembi amesema Tanzania imeendelea kuimarisha juhudi
za kupanua matumizi ya nishati safi ya kupikia kama sehemu ya ajenda
ya maendeleo endelevu.

Ameeleza kuwa mafanikio hayo yamechangiwa na utekelezaji wa maazimio
ya Mkutano wa Kwanza wa Afrika wa Nishati Safi ya Kupikia, ambapo
Tanzania ilishiriki kuhamasisha ahadi ya dola za Marekani bilioni 2.2
kwa ajili ya kuendeleza sekta hiyo barani Afrika.

Waziri Ndejembi amesisitiza kuwa mafanikio halisi yatapimwa kwa
utekelezaji wa vitendo na upanuzi wa huduma hususan maeneo ya vijijini
ambako matumizi ya kuni na mkaa bado ni makubwa.

Aidha, amebainisha kuwa Mei 2024, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, Mhe.Samia Suluhu Hassan, alizindua rasmi Mkakati wa Kitaifa
wa Nishati Safi ya Kupikia 2024–2034 unaolenga kuratibu sera, kanuni,
mifumo ya kifedha pamoja na ushiriki wa sekta binafsi ili kuongeza
matumizi ya nishati safi nchini.

“Kwa mwaka huu wa fedha, Serikali inatarajia kusambaza majiko banifu
200,000 na mitungi 450,000 ya gesi ya LPG kwa ruzuku, pamoja na kuanza
majaribio ya mfumo wa kulipia vifaa vya kupikia kwa umeme kupitia bili
za Shirika la Umeme Tanzania, ili kupunguza gharama za awali kwa
wananchi,” amesema.

Pia ameeleza kuwa Serikali imepiga marufuku matumizi ya kuni na mkaa
katika taasisi zinazohudumia zaidi ya watu 100, zikiwemo shule na
vituo vya afya, hatua inayolenga kupunguza uharibifu wa mazingira na
madhara ya kiafya yatokanayo na moshi wa ndani.

“Nishati safi ya kupikia inapaswa kuangaliwa pia kama sekta ya
kiuchumi inayoweza kuzalisha ajira katika uzalishaji, usambazaji na
matengenezo ya vifaa,” amesema Ndejembi huku akitoa wito kwa
wawekezaji kutumia fursa zilizopo.

Amesisitiza kuwa Tanzania itaendelea kushirikiana na wadau wa
maendeleo wa ndani na kimataifa ili kuhakikisha malengo ya upatikanaji
wa nishati safi ya kupikia yanafikiwa kwa kiwango kikubwa na endelevu,
sambamba na jitihada za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi na
kuboresha ustawi wa wananchi.

Kwa mujibu wa IEA, Afrika inaweza kufikia upatikanaji wa nishati safi
ya kupikia kwa wote ifikapo mwaka 2040, lakini mafanikio hayo
yanahitaji uwekezaji wa takribani dola bilioni mbili kila mwaka.

No comments:

Post a Comment