KAMATI YA MIUNDOMBINU YAPITISHA RANDAMA YA BAJETI WIZARA YA UJENZI 2026/2027. - OKULY BLOG

Breaking

Music

Header ADS

Tuesday, March 24, 2026

KAMATI YA MIUNDOMBINU YAPITISHA RANDAMA YA BAJETI WIZARA YA UJENZI 2026/2027.


Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu, imepitisha Randama ya Mpango na Bajeti ya Matumizi ya Kawaida na Mpango wa Maendeleo kwa mwaka wa fedha 2026/2027 ya Wizara ya Ujenzi hatua inayotajwa kuwa muhimu katika kuendeleza kasi ya uboreshaji wa miundombinu nchini.

Akizungumza jijini Dodoma Machi 24, 2026, Mwenyekiti wa kamati hiyo, Mhe. Selemani Kakoso, alisema uamuzi huo unaenda sambamba na dhamira ya kuhakikisha miundombinu ya kisasa inaendelea kujengwa na kuboreshwa ili kuchochea maendeleo ya kiuchumi kwa wananchi na Taifa kwa ujumla.

Katika hatua nyingine, Kamati hiyo imeipongeza Wizara ya Ujenzi kwa juhudi zake za kubuni na kutekeleza mikakati ya kupunguza msongamano wa magari, hususan katika majiji makubwa. Miongoni mwa miradi iliyotajwa ni pamoja na ujenzi wa barabara za juu (flyovers) katika jiji la Dar es Salaam pamoja na ujenzi wa interchange katika jiji la Dodoma.



Kwa upande wake, Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega ameishukuru Kamati hiyo kwa kuidhinisha randama hiyo na kuahidi kuwa Wizara itaendelea kusimamia kwa karibu utekelezaji wa miradi ya kimkakati ili kuhakikisha inakamilika kwa viwango bora na kuleta manufaa kwa wananchi.

Aidha, Ulega ameieleza Kamati kuwa Wizara inaendelea na hatua mbalimbali za utekelezaji wa miradi ya barabara iliyopangwa kutekelezwa kwa utaratibu wa Ushirikiano wa Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP) ikiwemo barabara ya Kibaha - Chalinze (km 78.9) na Chalinze - Morogoro (km 84.9).

Sambamba na hilo, Wizara imepanga kuendeleza ujenzi wa barabara za mzunguko wa ndani wa jiji la Dodoma, ikiwa ni jitihada za kupunguza msongamano wa magari. Miradi hiyo inahusisha barabara za Dodoma–Iringa, Dodoma–Singida, Dodoma–Arusha na Dodoma–Chamwino, ambapo kwa sasa ipo katika hatua za mwisho za kuwapata wakandarasi kwa ajili ya kuanza utekelezaji.




No comments:

Post a Comment