MIRADI YA DHARURA TABORA YAFIKIA ASILIMIA 80 - OKULY BLOG

Breaking

Music

Header ADS

Monday, June 8, 2026

MIRADI YA DHARURA TABORA YAFIKIA ASILIMIA 80


‎Na Mwandishi Wetu - Tabora

‎Mkoa wa Tabora umefikia asilimia 80 ya utekelezaji wa miradi ya matengenezo ya dharura inayofadhiliwa kupitia Mfuko wa Dharura (CERC) huku zaidi ya bilioni 1.6 zikitumika kurejesha mawasiliano na kuboresha miundombinu katika wilaya tatu za mkoa huo.
‎Meneja wa Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) mkoa wa Tabora Mhandisi Lusako Kilembe alisema miradi hiyo inaendelea vizuri na inatarajiwa kukamilika ifikapo Septemba mwaka huu.
‎Alisema miradi ya CERC inatekelezwa katika manispaa ya Tabora, wilaya ya Urambo pamoja na Sikonge ikihusisha ujenzi na ukarabati wa barabara, madaraja pamoja na makalavati yaliyoathiriwa na mafuriko.
‎"Tutahakikisha miradi yote inakamilika kwa wakati ifikapo Septemba mwaka huu. Miundombinu hii ni muhimu kwa maendeleo ya wananchi kwani itarejesha mawasiliano na kurahisisha usafirishaji wa mazao kutoka mashambani kwenda sokoni", alisema Mhandisi Kilembe.
‎Alibainisha kuwa kukamilika kwa miradi hiyo kutachochea shughuli za kiuchumi na kuboresha huduma za kijamii kwa wananchi wa maeneo husika.
‎Akizungumzia Daraja la Ndovelwa, alisema eneo hilo lilikuwa likikumbwa na changamoto kubwa wakati wa mvua kutokana na maji kujaa kwani eneo hilo ni mbuga hali iliyowafanya wananchi kushindwa kuvuka kwa usalama.
‎"Awali wananchi walikuwa wakihatarisha maisha yao kuvuka eneo hili wakati wa mvua kubwa. Kukamilika kwa daraja hili kutaondoa adha hiyo na kuimarisha mawasiliano kati ya Igalula na Goweko ambako kuna shughuli nyingi za kijamii na kiuchumi ikiwemo kilimo", alisema.
‎Naye, Meneja wa TARURA Manispaa ya Tabora, Mhandisi Vicent Manyama alisema mradi huo kwa sasa upo katika hatua ya mwisho ya uangalizi na umefikia asilimia 97 ya utekelezaji hadi sasa jumla ya shilingi milioni 272.8 zimelipwa kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huo.
‎Meneja huyo ameishukuru serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwezesha upatikanaji wa fedha ambazo zimekuwa chachu ya utekelezaji wa matengenezo na uboreshaji wa miundombinu ya barabara ambayo imesaidia kuboresha upatikanaji wa huduma za kijamii na kuchochea shughuli za kiuchumi kwa wananchi.
‎Daraja hilo ni miongoni mwa miradi ya kimkakati inayotekelezwa na TARURA kwa lengo la kuimarisha mtandao wa usafiri na usafirishaji katika mkoa wa Tabora.

No comments:

Post a Comment