Na OWM – TAMISEMI, Lushoto
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) ambaye ofisi yake ina jukumu la kusimamia, kuratibu na kuendeleza michezo na sanaa katika shule za msingi na sekondari, ameacha somo la vitendo kwa vijana kuthamini na kuendeleza vipaji vyao baada ya kuonesha umahiri wa kupiga ngoma na kuimba mubashara akiwa na Bendi ya TOT wakati wa mapokezi ya Mwenge wa Uhuru wilayani Lushoto Juni 26, 2026.
Tukio hilo ambalo lililopokelewa kwa shamrashamra, vigelegele na makofi kutoka kwa wananchi, limebeba ujumbe muhimu kwa vijana wa Tanzania, hususan washiriki wa mashindano ya UMITASHUMTA na UMISSETA, kwamba vipaji havipaswi kuonekana kama burudani ya muda mfupi, bali ni rasilimali yenye uwezo wa kufungua fursa za ajira, kujiajiri na kutangaza utamaduni wa taifa.
Kwa miaka mingi, mashindano ya UMITASHUMTA na UMISSETA yameendelea kuwa jukwaa muhimu ya kugundua na kukuza vipaji vya uimbaji, upigaji ngoma, muziki, maigizo na sanaa nyingine, hivyo kitendo cha Prof. Shemdoe kushiriki muziki kwa kujiamini kinaonesha kuwa kipaji hakizuiliwi na umri, taaluma au nafasi ya uongozi, bali kinahitaji kuthaminiwa, kufanyiwa mazoezi na kuendelezwa.
Kwa vijana wanaobahatika kushiriki mashindano ya UMITASHUMTA na UMISSETA, Prof. Shemdoe amewaachia ujumbe huu : aminini vipaji vyenu, vifanyieni kazi kwa nidhamu na bidii, kwani vinaweza kuwa daraja la kufikia ndoto zenu, kuchangia maendeleo ya Taifa na kuutangaza utamaduni wa Tanzania duniani.










No comments:
Post a Comment