Na Okuly Julius Dodoma
MAKAMU wa Rais Dk philip Mpango ameitaka benki ya NMB kuongeza ubunifu ili iweze kuwafikia watu wengi hususani waishio vijijini,Wenye ulemevu na kusaidia ajira kwa vijana pamoja na kujikita katika utunzaji wa mazingira ili kuendelea kuwa benki bora hapa nchini.
Dk Mpango amesema benki hiyo imeendelea kuiheshimisha Serikali kwa kuonyesha namna gani inavyokuwa kimtaji na kuwajali wateja wake huku akisema kuwa benki hiyo imefanya siku yake na Serikali nzima kuwa yenye furaha.
"Nimefurahi sana maana kipindi kama hiki mwaka jana nilipopokea gawio la Sh20.8 bilioni ikiwa ni faida ya 2020 na niliwataka mkaongeze ubunifu na nguvu kubwa ili tukikutane tena mje na gawio nono na kweli leo mmenidhihirishia kwa vitendo kuwa mmefanyia kazi maagizo yale na mmekuja na gawio nono kweli kweli" Dk.Mpango
Na kuongeza “Hata nitakapokwenda kumpokea Mheshimiwa Rais, hili litakuwa ni jambo la kwanza kumuambia, moyo wangu umeburudika sana, mmenifurahisha sana nasema hongereni sana,” Dk Mpango.
Kwa gawio hilo, inafanya NMB ndani ya kipindi cha miaka mitano kuwa wametoa jumla ya Sh80.544 bilioni kwa serikali.
Kwa upande mwingine Dk Mpango ameagiza kwa viongozi wa mabenki na mwanasheria Mkuu wa Serikali kukaa pamoja na kuzungumza namna ya kupunguza riba ambalo alidai limekuwa ni donda ndugu na kwamba ndani ya mwaka mmoja watoe majibu.
Akitoa taarifa yake kwa Makamu wa Rais, Afisa Mtendaji Mkuu wa NMB Ruth Zaipuna amesema kuwa Faida ya Benki baada ya kodi katika kipindi cha 2021 iliongezeka kwa asilimia 41 hadi kufikia Sh290 bilioni.
Kiasi hicho ni kikubwa ukilinganisha na Sh206 bilioni ya mwaka 2020 ambapo idadi ya idadi ya akaunti za wateja iliongezeka hadi kufikia milioni tano ikilinganishwa na milioni nne za 2020.
“Katika kuhakikisha Benki inaendelea kuwa na maendeleo endelevu,tumeweza kuongeza mtaji wa Benki hadi Sh1.3 trilioni na Benki iliendelea kuwa na ufanisi, na kuweka rekodi ya uwiano wa gharama za uendeshaji na mapato, kufikia asilimia 46,” alisema Zaipuna.
Afisa huyo amesema kwa mwaka 2021, Benki ilipata Tuzo saba za kimataifa, ikiwemo ya benki bora nchini kwa mwaka wa tisa mfululizo ambayo iliyotolewa na Jarida la Kimataifa la Euromoney.
Kwa mujibu wa Mtendaji huyo, hadi mwishoni mwa 2021, jumla ya mikopo ya Sh4.3 trilioni ilikuwa imetolewa kwa wakulima, wafanyabiashara wadogowadogo na wa Kati na watu binafsi.
Akizungumzia mafanikio ya benki, amesema yalitokana na uwekezaji katika mifumo ya kidijitali, huduma za wakala, ambazo ziliongezeka na kufikia mawakala 10,194 ukilinganisha na 8,410 waliokuwepo 2020.
Naye Mwenyekiti wa bodi ya wadhamini ya NMB Dk Edwin Mhede amesema ongezeko la faida kwa benki hiyo linatokana na uimara na umadhubuti wa uongozi na kwamba wanajivunia kuwa na Mtendaji Mkuu Ruth Zaipuna.
Alitaja mafanikio kwa kipindi cha miaka mitano mfululizo kuwa yamekuwa yakipanda kila mwaka ambapo 2020 walitoa gawio la Sh20.8 bilioni, huku 2019 zikiwa Sh15.6 bilioni.
Dk Mhede amesema gawio kwa mwaka wa 2022 wanatarajia kuwa na gawio nono zaidi kwani kwa kipindi cha miezi mitatu ya mwanzo wamepata faida kubwa inayolingana na faida ya mwaka mzima katika kipindi cha miaka ya nyuma kutokana na ubunifu uliofanywa na watumishi wa benki.
No comments:
Post a Comment