TANZANIA NA IFC ZAJADILI USHIRIKIANO WA SEKTA YA UMMA NA SEKTA BINAFSI KWA MAENDELEO YA NCHI - OKULY BLOG

Breaking

Music

Header ADS

Wednesday, March 25, 2026

TANZANIA NA IFC ZAJADILI USHIRIKIANO WA SEKTA YA UMMA NA SEKTA BINAFSI KWA MAENDELEO YA NCHI

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akiagana na Mkurugenzi wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IFC) Kanda ya Afrika Mashariki, Bi. Mary Porter Peschka, baada ya kukutana na kuzungumza katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaam, kuhusu masuala mbalimbali ya kushirikiana katika ili kuongeza uwekezaji wa sekta binafsi, kupanua miundombinu na kuharakisha mpango wa taifa wa mabadiliko ya nishati chini ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 (DIRA 2050).
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akizungumza jambo wakati akiongoza kikao na ujumbe kutoka Shirika la Fedha la Kimataifa (IFC) Kanda ya Afrika Mashariki, ukiongozwa na Mkurugenzi wake, Bi. Mary Porter Peschka, baada ya kukutana na kuzungumza katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaam, ambapo walijadili masuala mbalimbali ya kushirikiana katika ili kuongeza uwekezaji wa sekta binafsi, kupanua miundombinu na kuharakisha mpango wa taifa wa mabadiliko ya nishati chini ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 (DIRA 2050).
Mkurugenzi wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IFC) Kanda ya Afrika Mashariki, Bi. Mary Porter Peschka, akizungumza jambo wakati wa alipoongoza ujumbe wa IFC kufanya mazungumzo na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (hayupo pichani), katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaam, ambapo walijadili masuala mbalimbali ya kushirikiana katika ili kuongeza uwekezaji wa sekta binafsi, kupanua miundombinu na kuharakisha mpango wa taifa wa mabadiliko ya nishati chini ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 (DIRA 2050).
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akiongoza kikao chake na ujumbe kutoka Shirika la Fedha la Kimataifa (IFC) Kanda ya Afrika Mashariki, ukiongozwa na Mkurugenzi wake, Bi. Mary Porter Peschka, baada ya kukutana na kuzungumza katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaam, ambapo walijadili masuala mbalimbali ya kushirikiana katika ili kuongeza uwekezaji wa sekta binafsi, kupanua miundombinu na kuharakisha mpango wa taifa wa mabadiliko ya nishati chini ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 (DIRA 2050).
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (Katikati), Mkurugenzi wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IFC) Kanda ya Afrika Mashariki, Bi. Mary Porter Peschka, na maafisa waandamizi kutoka Wizara ya Fedha, Wizara ya Nishati, Kituo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPPC), pamoja na wawakilishi wa IFC, wakiwa katika picha ya pamoja baada ya kukutana na kufanya mazungumzo katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaam, kuhusu masuala mbalimbali ya kushirikiana katika ili kuongeza uwekezaji wa sekta binafsi, kupanua miundombinu na kuharakisha mpango wa taifa wa mabadiliko ya nishati chini ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 (DIRA 2050).


(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF, Dar es Salaam)


Na Benny Mwaipaja, Dar es Salaam


Serikali ya Tanzania imerejea tena dhamira yake ya kushirikiana kwa karibu na Shirika la Fedha la Kimataifa (IFC) ili kuongeza uwekezaji wa sekta binafsi, kupanua miundombinu na kuharakisha Mpango wa Taifa wa mabadiliko ya nishati chini ya Dira ya Taifa ya Maendeleo (DIRA 2050).

Akizungumza katika kikao na Mkurugenzi wa IFC Kanda ya Afrika Mashariki, Bi. Mary Porter Peschka, Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), alisifu mchango wa muda mrefu wa IFC katika kukuza sekta binafsi nchini Tanzania, akisisitiza kuwa ushirikiano huo utaendelea kuwa muhimu katika kufanikisha malengo ya muda mrefu ya maendeleo ya taifa.

Mhe. Balozi Omar alibainisha mchango mkubwa wa IFC katika kukuza ukuaji wa sekta binafsi kupitia ufadhili wa fedha, ubunifu na programu za kujenga uwezo wa kitaasisi.

Alieleza kuwa utekelezaji wa DIRA 2050, unaokadiriwa kugharimu takribani dola za Marekani trilioni 1, utategemea kwa kiasi kikubwa uwekezaji wa sekta binafsi unaotarajiwa kuchangia zaidi ya asilimia 70 ya gharama za utekelezaji.
“Ushirikiano endelevu na IFC ni muhimu katika kuhamasisha rasilimali, kuchochea ushiriki wa sekta binafsi na kuhakikisha mageuzi ya kijamii na kiuchumi ya Tanzania yanafikiwa,” alisema Mhe. Balozi Omar.

Mhe. Balozi Omar pia alizungumzia mafanikio yaliyopatikana kupitia Mpango wa Taifa wa Nishati (Mission 300 Tanzania Energy Compact), unaolenga kuongeza upatikanaji wa umeme na nishati safi kufikia mwaka 2030.

Kati ya Januari 2025 na Januari 2026, upatikanaji wa umeme nchini umeongezeka kutoka asilimia 78.4 hadi 85.5, uunganishaji wa kaya kufikia gridi umeongezeka kutoka asilimia 46 hadi 52.1, na sehemu ya nishati inayotokana na vyanzo vinavyoweza kurejelewa imepanda kutoka asilimia 61.8 hadi 69.

Hata hivyo, Mhe. Balozi Omar alisisitiza haja ya kuendelea kuvutia uwekezaji zaidi ili kupanua huduma hasa vijijini na kukuza matumizi ya nishati safi kwa kupikia.

Aliitaka IFC kutumia utaalamu wake wa kimataifa kufadhili miradi ya kimkakati ya nishati kama mitambo ya umeme wa maji ya Kikonge, Ruhudji na Rumakali, pamoja na miradi ya jua, upepo na jotoardhi iliyomo ndani ya mpango huo.
Aidha, alieleza jitihada za serikali katika kuvutia mitaji ya sekta binafsi kupitia miradi ya Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPPs) ambapo Kituo cha Ubia Kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPPC) kimeandaa orodha ya kitaifa inayojumuisha miradi 113 iliyoko katika hatua mbalimbali za maandalizi na utekelezaji katika sekta muhimu ikiwemo usafiri, biashara, kazi, na kilimo. Miradi 10 muhimu inatarajiwa kuendelezwa katika mwaka wa fedha 2026/27, ikihitaji msaada wa kifedha kwa ajili ya maandalizi.

Mhe. Balozi Omar aliiomba IFC kutoa ushauri wa kitaalamu na msaada wa kitaasisi ili kusaidia PPPC na taasisi za serikali katika kuandaa miradi kulingana na viwango vya kimataifa.
“Kuimarisha uwezo wa taasisi zetu na kuoanisha miradi ya PPP na viwango bora vya kimataifa kutaimarisha imani ya wawekezaji na kuharakisha utekelezaji,” alisema Balozi Omar.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa IFC Kanda ya Afrika Mashariki, Bi. Mary Porter Peschka, amesema kuwa Taasisi yake ambayo ni miongoni mwa Taasisi zilizochini ya Benki ya Dunia, iko tayari kuendelea kushirikiana na Tanzania katika kukuza sekta binafsi katika Nyanja mbalimbali za kukuza biashara, nishati, kilimo biashara na uwekezaji ili kuinua maisha ya watu na uchumi wa Tanzania.

Kwa mujibu wa tathmini ya IFC ya mwaka 2025, taasisi hiyo imewekeza takribani dola milioni 197.4 katika nusu ya kwanza ya mwaka wa fedha 2026, kupitia mikopo ya muda mfupi iliyolenga kuchochea shughuli za sekta binafsi.
Kiasi cha uwekezaji wa IFC nchini Tanzania kimefikia dola milioni 315.9, ambapo asilimia 74 imeelekezwa katika sekta ya huduma za kifedha na asilimia 26 katika viwanda, kilimo-biashara, na huduma nyingine.

IFC pia inaunga mkono utekelezaji wa Mradi wa Usafiri wa Mabasi yaendayo Haraka (BRT) jijini Dar es Salaam kupitia huduma za ushauri wa PPP, pamoja na kutekeleza Mpango wa Kitaifa wa Jinsia (Gender Program) wenye thamani ya dola milioni 6.3 hadi mwaka 2028, unaolenga kuongeza ushiriki wa wanawake katika shughuli za kibiashara.
Kikao hicho kilihudhuriwa na maafisa waandamizi kutoka Wizara ya Fedha, Wizara ya Nishati, Kituo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPPC), pamoja na wawakilishi wa IFC.

No comments:

Post a Comment