MKOA WA NJOMBE KUSHIRIKIANA NA OMR, WIZARA YA MALIASILI KUDHIBITI MAJANGA YA MOTO - OKULY BLOG

Breaking

Music

Header ADS

Monday, April 27, 2026

MKOA WA NJOMBE KUSHIRIKIANA NA OMR, WIZARA YA MALIASILI KUDHIBITI MAJANGA YA MOTO


Mkuu wa Mkoa wa Njombe Mhe. Antony Mtaka amesema Mkoa huo umepanga kushirikiana na Ofisi ya Makamu wa Rais na Wizara ya Maliasili na Utalii ili kukabiliana na majanga ya moto yanayotokea mara kwa mara katika mashamba ya miti katika maeneo ya vijijini.

Mhe. Mtaka ametoa kauli hiyo Aprili 27, 2025 wakati akioongoza Wanamichezo kutoka Wizara, Idara, Taasisi za Umma na Binafsi katika zoezi la upandaji miti kupitia kampeni maalum ijulikanayo “27 ya Kijani, Mti wa Mama” katika tukio lililofanyika katika Ofisi za Makao Makuu Mkoa huo.

Mhe. Mtaka amesema matukio ya majanga ya moto Mkoani humo yamekuwa yakijitokeza mara na hivyo kusababisha hasara kuwa kwa wawekezaji, wafanyabiashara na wananchi wanaojihusisha na biashara ya mazao ya miti ikiwemo mbao na nguzo za umeme.

“Kuanzia mwaka 2021-2026 matukio ya majanga ya moto hapa Njombe yamesababisha hasara ya zaidi ya Shilingi Bilioni 200 na hatua hii umetufundisha kuchukua hatua za tahadhari katika kukabiliana na majanga hayo” amesema Mhe. Mtaka.

Amesema kufuatia hali hiyo, Sekretarieti ya Mkoa huo imepanga kushirikiana na Ofisi ya Makamu wa Rais na Wizara ya Maliasili kwa ajili ya kuandaa kampeni ya elimu kwa umma ili kuwaelimisha wananchi wa maeneo ya vijiji namna bora ya kukabiliana na majanga ya moto.

Ameongeza kuwa mbali na kuandaa mpango huo, Ofisi yake kwa kushirikiana na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) tayari wameanza kuendesha kampeni ya elimu kwa umma kuhusu uzuiaji wa majanga ya moto.

Amesema kutokana na fursa zilizopo Mkoani humo katika biashara ya miti, Ofisi yake imeendelea kushirikiana na wadau kutoka taasisi ya panda miti kibiashara ambayo imekusudia kuwafikia wananchi na kamati za mazingira za vijiji.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano ya Michezo ya Mei Mosi, Roselyn Massam amesema kamati hiyo na wanamichezo itaendelea kuunga mkono kwa vitendo juhudi za serikali katika masuala ya uhifadhi wa mazingira ikiwemo kushiriki zoezi la upandaji miti.

Tumeshiriki kwa wingi katika zoezi hili ili kuonesha msisitizo wa wanamichezo kuhusu utunzaji wa mazingira ili kutekeleza maelekezo ya Mhe Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika upandaji wa miti” amesema Bi. Massam.

Kwa upande wake Katibu wa Klabu ya Michezo Ofisi ya Makamu wa Rais, Marwa Nyaisawa amesema Ofisi hiyo imeshiriki zoezi hilo la upandaji miti ili kuhamasisha wanamichezo wanaoshiriki Mashindano ya Michezo ya Mei Mosi kuunga mkono juhudi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

“Tumeshirikiana na wanamichezo wenzetu ili kuhamasisha kampeni hii ya upandaji miti ya 27 ya kijani, Mti wa Mama na pia kuwajengea utamaduni wa kupanda miti maofisi yao na jamii inayowazunguka” amesema Nyaisawa.

Nae Mwenyekiti wa Klabu ya Michezo kutoka Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Fortunatus Patrick amesema zoezi hilo la upandaji miti limekuja katika kipindi mwafaka kwa taasisi hususani katika kipindi hiki ambapo inatimiza miaka 40 tangu kuanzishwa kwake.

“Katika kutimiza miaka 40 ya NEMC tumekuwa tukiendelea kuelimisha wananchi kuhusu umuhimu wa kutunza mazingira hususani kupanda miti kwani kama tunavyotambua bila miti hakuna uhai wa binadamu na viumbe hai wengine” amesema Fortunatus.

Zoezi hilo la upandaji miti limehusisha Viongozi mbalimbali kutoka Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Nchini (TUCTA), Kamati ya Michezo ya Mei Mosi Taifa, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya Maadhimisho ya Sikukuu ya Wafanyakazi Duniani, 2026 (Mei Mosi) yatakayofanyika Mkoani humo.

Kauli Mbiu ya maadhimisho ya Mei Mosi, 2026 inasema “Kazi Zenye Staha ni nguzo endelevu katika utekelezaji wa Dira 2050”





No comments:

Post a Comment