
Na Okuly Julius, OKULY BLOG, DODOMA
Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imeomba kuidhinishiwa jumla ya Shilingi trilioni 2.398 kwa ajili ya utekelezaji wa majukumu na miradi mbalimbali ya maendeleo katika mwaka wa fedha 2026/2027.
Hayo yameelezwa bungeni jijini Dodoma na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda wakati akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/2027.
Prof. Mkenda amesema kati ya fedha hizo, Shilingi 2,394,423,829,000 zimeombwa kwa ajili ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia (Fungu 46), ambapo Shilingi 697,841,881,000 ni kwa matumizi ya kawaida.
Amefafanua kuwa ndani ya fedha za matumizi ya kawaida, Shilingi 648,082,352,000 zitatumika kwa mishahara ya watumishi huku Shilingi 49,759,529,000 zikielekezwa kwenye matumizi mengineyo.
Aidha, amesema Shilingi 1,696,581,948,000 zinaombwa kwa ajili ya miradi ya maendeleo, ambapo Shilingi 1,337,249,000,000 ni fedha za ndani na Shilingi 359,332,948,000 ni fedha kutoka kwa washirika wa maendeleo.
Katika hatua nyingine, Waziri huyo amesema Wizara kupitia Tume ya Taifa ya UNESCO (Fungu 18) imeomba kuidhinishiwa Shilingi 3,866,993,000 kwa matumizi ya kawaida.
Kwa mujibu wa Prof. Mkenda, kati ya fedha hizo za UNESCO, Shilingi 1,335,020,000 ni kwa mishahara na Shilingi 2,531,973,000 ni kwa matumizi mengineyo.
Ameomba Bunge kupokea, kujadili na kupitisha makadirio hayo ya bajeti yenye jumla ya Shilingi 2,398,290,822,000 kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli za Wizara katika mwaka wa fedha 2026/2027.

No comments:
Post a Comment