Na Mwandishi Wetu - Dodoma
Serikali ya Tanzania kupitia Wizara ya Madini na Shirika la Ushirikiano wa Kimataifa la Japan (JICA) zimekubaliana kupanua wigo wa ushirikiano kwa kubainisha maeneo ya kipaumbele yatakayofadhiliwa kupitia JICA kwa msaada wa Serikali ya Japan ikiwemo utafiti wa madini muhimu na mkakati.
Hayo yamebainishwa Juni 25, 2026 jijini Dodoma katika kikao kilicholenga kuimarisha ushirikiano katika maendeleo ya Sekta ya Madini nchini.
Akizungumza katika kikao hicho, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Madini Msafiri Mbibo amesema ushirikiano na taasisi hiyo ni wa muda mrefu ambao kupitia JICA zaidi ya wataalamu 30 wa Sekta ya Madini wamepatiwa mafunzo nchini Japan yaliyowajengea uwezo na kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu ya Wizara na taasisi zake na kueleza kwamba, ushirikiano huo utaendelea kuimarishwa kwa manufaa ya Tanzania na Japan.
Kwa upande wake, Mwakilishi Mkazi wa JICA nchini Tanzania, Dkt. Katsuyika Kuge, amesema pamoja na utekelezaji wa Mradi wa Kizuna unaojenga uwezo wa wataalamu wa sekta hiyo, JICA inapanga kupanua ushirikiano katika maeneo ya utafiti wa madini muhimu na madini mkakati, ikiwemo shaba, kinywe (graphite), beryllium na madini adimu ya Heavy Rare Earth Elements (Heavy REE).
Aidha, Dkt. amefafanua kuwa, kwa kuanzingatia vipaumbele vya JICA, kwa kuanzia, kipaumbele cha utafiti kitajikita kwenye eneo la madini kinywe na beryllium.
‘’ Ninaipongeza Serikali ya Tanzania kwa usimamizi mzuri wa Sekta ya Madini, pamoja na utekelezaji wa mradi wa Kizuna unaowajengea uwezo watalaam wa Sekta ya madini, JICA inapanga kupanua ushirikiano katika maeneo ya utafiti wa madini muhimu na mkakati,’’ amesema Dkt.Kuge.






No comments:
Post a Comment