KIWANDA KIKUBWA CHA KUCHAKATA MCHANGA MZITO WA BAHARINI(HMS) BARANI AFRIKA KUJENGWA PANGANI,TANGA - OKULY BLOG

Breaking

Music

Header ADS

Monday, September 14, 2026

KIWANDA KIKUBWA CHA KUCHAKATA MCHANGA MZITO WA BAHARINI(HMS) BARANI AFRIKA KUJENGWA PANGANI,TANGA


Na Mwandishi Wetu - Chengdu,China


Kampuni ya Shenghe Resources ya China imeanza ujenzi wa kiwanda kikubwa cha kuchakata madini madini ya mchanga mzito wa baharini (𝙃𝙚𝙖𝙫𝙮 𝙈𝙞𝙣𝙚𝙧𝙖𝙡 𝙎𝙖𝙣𝙙𝙨) katika eneo la Tajiri,Wilaya ya Pangani Mkoani Tanga ambapo kampuni hii inatekeleza mradi mkubwa wa uchimbaji wa madini tembo.

Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Kampuni ya Shenghe Ndg. Xie Bing wakati wa ziara ya Waziri wa Madini Mh. Anthony Mavunde kutembelea na kujionea shughuli mbalimbali za uongezaji thamani madini zinazofanywa kampuni hiyo.

Akizungumza katika ziara hiyo Ndg. Bing amesema kwa Bara la Afrika wana miradi ya madini hayo katika nchi za Msumbiji, Afrika ya Kusini na Madagascar lakini wameichagua Tanzania kuwa ndio kitovu cha uchakataji madini hayo barani Afrika na sasa wameanza ujenzi wa Kiwanda cha kuchakata madini hayo(𝙈𝙞𝙣𝙚𝙧𝙖𝙡 𝙎𝙚𝙥𝙖𝙧𝙖𝙩𝙞𝙤𝙣 𝙋𝙡𝙖𝙣𝙩) wilayani Pangani,Tanga na kuahidi kukamilisha ndani ya muda mfupi ujao ambapo malighafi kutoka nchi nyingine za Afrika zitaletwa Tanzania kwa ajili ya uchakataji wake na kuongezea thamani.

Aidha,Ndg. Bing ameipongeza Serikali ya Tanzania chini ya uongozi wa Mh. Rais Samia S. Hassan kwa mazingira rafiki ya uwekezaji ambayo yamewavutia kuja kuwekeza Tanzania.

Akizungumza katika ziara hiyo,Waziri wa Madini Mh. Anthony Mavunde amepongeza maamuzi hayo makubwa ya Kampuni ya Shenghe ambayo yanaendana na sera ya Madini na Sheria ya Madini ya takwa la uongezaji thamani madini nchini na kusema hatua hiyo itachochea upatikanaji wa Ajira,Kuongezeka kwa mapato na kukua kwa teknolojia katika eneo la uchakataji madini.

Aidha Waziri Mavunde ameitaka Kampuni ya Shenghe kuhakikisha inakamilisha ujenzi wa kiwanda hicho kwa wakati na pia inamalizia malipo ya fidia kwa maeneo machache yaliyobaki.

No comments:

Post a Comment